KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Vincent Mashinji amesema, ‘tayari tumemjibu msajili.’ Anaandika Regina Mkonde…(endelea).
Amesema, chama hicho kimejibu barua ya msajili leo tarehe 7 Oktoba 2019, na kwamba kwenye barua hiyo, wameandika tarehe maalum ya kufanya uchaguzi wa viongozi.
“Tumepeleka barua ya majibu asubuhi ya leo. Ratiba yetu iko pale pale, tarehe 18 Desemba 2019 tutafanya uchaguzi wa viongozi,” amesema Dk. Mashinji.
Katibu Mkuu huyo wa Chadema alikuwa akijibu swali la mwandishi wa MwanaHalisi Online, lililohoji hatua zilizofikiwa na chama hicho.
Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, tarehe 1 Oktoba 2019 iliiandikia barua Chadema ili kueleza sabababu za kutofanya uchaguzi wa viongozi wa chama, na kukipa siku siku kujibu barua hiyo.
Barua hiyo ilieleza kuwa, Chadema kimevunja sheria kwa kutoitisha mkutano mkuu pamoja na kutofanya uchaguzi wa viongozi wapya, licha ya kipindi cha uongozi wa viongozi wake kikatiba kuisha.
Sehemu ya barua hiyo ilieleza kwamba, Chadema kinapaswa kuwasilisha maelezo yake kwa Msajili wa Vyama vya Siasa, kwanini kisichukuliwe hatua za kisheria kwa kukiuka Sheria ya Vyama vya Siasa, Katiba na Kanuni za hicho.
Barua hiyo ya msajili iliitaka Chadema kuwasilisha maelezo yake ndani ya siku saba, ambapo mwisho ilikuwa leo saa 9.30 mchana.
Leave a comment