CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimejibu mapigo baada ya aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Vincent Mashinji kuhamia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Kupitia taarifa aliyoitoa Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje wa chama hicho, John Mrema amesema walitegemea kusikia Mashinji amehama chama na kwamba hajaacha pengo.
“Taarifa za Dk. Mashinji kujiunga na CCM hazijatushtua, tulikuwa tunazitegemea, tunajua ni kati ya watu ambao walishajipanga kuondoka muda mrefu, ndio maana interejensia ya chama ikashauri mamlaka yake ya uteuzi ambaye ni Mwenyekiti wa Chama Freeman Mbowe asimteue tena Mashinji kuwa Katibu Mkuu,” amesema Mrema.
Aidha, ameeleza kuwa mwanachama huyo kabla ya kuondoka kuhamia CCM alitengeneza wagombea wake ambao wote nao walishaunga mkono juhudi.
“Wakati anapanga mipango ya kuondoka alitengeneza mgombea urais wake ambaye ni Mzee Sumaye naye amesharudi CCM, akamtengeneza Mwenyekiti wake wa chama ambaye ni Cecil Mwambe naye amesharejea CCM na yeye amefuata na tunategemea wengine wengi waliokuwa kwenye kundi lake watafuata,” amesema.
Mrema amesema wapo wengi waliopanga kuunga mkono juhudi kuhamia CCM hasa katika kipindi hiki cha mapambano ya kudai tume huru ili kuhamisha mjadala.
“Kuondoka kwake hatuwezi kusema kwamba ni pengo kwa sababu lingekuwa pengo ingekuwa kwa wakati wa Dk. Slaa ambaye alikaa madarakani muda mrefu kuliko wote,” amesema.
Dk. Mashinji ametangaza kujiunga na CCM leo tarehe 18 Februari 2020 huku akieleza kuwa ‘Chadema sio taasisi ya umma kama ambavyo watu wanafikiria bali ni kampuni binafsi ya Freeman Mbowe.
“Nimeona tuache malumbano asubuhi na jioni. Nije Lumumba kuongea na wenzangu ili nione ninaweza kupata fursa ya kujiunga na CCM kwa madhumuni ya kunilea na kunikuza. Ninahitaji kuendelea kutoa mchango wangu kwa maendeleo ya taifa,” amesema Mashinji.
Dk. Mashinji anaweka historia ya kuwa Katibu Mkuu wa kwanza kukaa madarakani kwa muda mfupi kuliko wote, baada ya kuhudumu kwa miaka mitatu, ukilinganisha na Bob Makani, Amani Kaburu na hata Dk. Wilbroad Slaa.
Leave a comment