UONGOZI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kanda ya kati pamoja na uongozi wa Chadema mkoa wa Morogoro wameungana kufanya maombi ya kumwombea mbunge wa Singida Mashariki , Tundu Lissu pamoja na kuhamasisha michango kwa ajili ya matibabu.
Maombi hayo yalifanywa na uongozi wa kanda ya kati pamoja na uongozi wa Chadema mkoa wa Morogoro huku wakilaani vitendo vya polisi kuendelea kuwakamata na kuwanyanyasa wapinzani.
Viongozi hao wa Chadema wamesema polisi wameshindwa kuwakamata ama kutoa taarifa za watu ambao wanafanya uhalifu lakini hawabainiki.
Awali viongozi hao wa chadema kanda ya kati pamoja na mkoa Morogoro walikutana kwa lengo la kuweka uongozi wa Chadema msingi ambao utafanya kazi ya kuratibu shughuli zote za kuimarisha chama ikiwa ni pamoja na kukijenga.
Akifungua kikao hicho mwenyekiti wa Chadema kanda ya kati, Alphonce Mbassa amesema kuwa licha ya kuwepo changamoto kubwa ya kufanya siasa kwa sasa kutokana na serikali kwa kutumia vyombo vya dola kuukandamiza upinzania, lakini ni lazima chama kiweke mikakati ya kuimarisha.
Akizungumzia kuhusu suala la polisi kuwakamata viongozi wakiwa katika shughuli zao za kawaida, Mbassa amesema umefika wakati wa wanachama kutambua kwamba wanatakiwa kutumia nafasi zao kufanya siasa bila kuwa na uoga.
“Nataka niwaeleze viongozi na wapenzi wa Chadema kanda ya kati, mkoa wa Morogoro pamoja na taifa kwa ujumla, wote mnajua kuwa kiongozi wetu Tundu Lissu alipigwa risasi, lakini imekuwa shida sana kuandaa maombi, kuvaa tishert ni shida hata kufanya michango imeoneekana kuwa ni jambo la kisiasa.
“Mkiona hali kama hiyo sasa hapo ndo pakujua kuwa serikali inaelekea kuanguka na vyama vya upinzani kuchukua dola” amesem Mbassa.
Leave a comment