KINYANG’ANYIRO cha uchaguzi mkuu ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeanza kukimega chama hicho. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Mbunge wa Ukonga (CHADEMA), Mwita Mwaikabe Waitara, ameamua kuondoka chama hicho na kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Waitara, alikuwa mmoja wa viongozi wandamizi ndani ya Chadema ambao wanapinga Freeman Mbowe, kuendelea kugombea uenyekiti wa chama hicho katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwaka kesho.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya chama hicho, tayari Mbowe ameunda “mtandao” kwa lengo la kumtetea na kuhakikisha anagombea kwa “gharama yeyote” nafasi hiyo na kushinda.
Akitangaza uamuzi wake wa kuondoka Chadema, leo Jumamosi, tarehe 28 Julai, ofisi ndogo ya CCM, Lumumba, jijini Dar es Salaam, Waitara amesema, “nimeamua kuondoka Chadema kwa kuwa hakuna demokrasia.”
Waitara amepokelewa ndani ya chama hicho ambacho aliwahi kuwa katibu wa Umoja wa Vijana (UV-CCM), mkoani Tanga na Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC), Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole.
“Ugomvi wangu na Mbowe hivi sasa, ni uchaguzi wa ndani ya chama. Yeye anataka kuwa mwenyekiti na ameapa kumshughulikia yeyote anayepinga mradi wake huu,” ameeleza Waitara.
Amesema, “mimi nilisema huyu mtu ameongoza chama miaka 20. Anapaswa kupumzika. Lakini yeye amekusanya wapambe wanaomtetea; na ndani ya chama sioni demokrasia, bali kuna vitu vya kupachika pachika.”
Anaongeza, “lakini pili kuna matumizi mabaya ya ruzuku. Chadema kinapata ruzuku ya Sh. 360 milioni, kila mwezi. Lakini fedha zote zinaliwa na wakubwa pale makao makuu; na kwamba hakuna anayeruhusiwa kuhoji chochote.”
Kwa mujibu wa Waitara, akiwa mbunge wa Chadema, amepata changamoto mbili. Namna ya kufanya kazi na Chadema na jambo la pili, ni namna ya kushirikiana na serikali kuleta maendeleo.
Leave a comment