CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kinategemea kupokea wageni zaidi ya 1,500 katika mji wa Dodoma ambao watahudhuria vikao vya kamati kuu na baraza kuu la chama hicho, anaandika Dany Tibason.
Mbali na kupokea ugeni huo Chadema kimetangaza kuufunika mji wa Dodoma kwa kutundika bendera kila kona ya mji pamoja na nje ya mji kuanzia kesho wakati wa kufanyika kwa kikao cha Kamati Kuu na Baraza Kuu Chadema Taifa ambapo baraza hilo kikatiba ufanyika mara moja kwa mwaka.
Baraza kuu linafanyika kwa mara ya kwanza mkoani Dodoma ambapo mwaka jana baraza hilo lilifanyika jijini Mwanza.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Kati, Alphonce Mbassa amesema chama hicho kinatarajia kufanya mkutano wa baraza kuu katika mji wa Dodoma.
Mwenyekiti huyo wa kanda akizungumza na vyombo vya habari, amesema kesho kutakuwepo na kikao cha Sekretalieti, kwa ajili ya maandalizi ya Kamati Kuu.
Amesema ofisi ya Katibu Mkuu wa Chadema ndiyo itakayokuwa inafanya kamati ya sekretalieti ambapo Mei 26, mwaka huu wajumbe wote watakaa na kujadili na kuandaa agenda ambazo zitapelekwa katika baraza kuu.
Akiendelea kufafanua amesema 27 ndipo kutakuwaezo na kikao kikubwa cha mkutano wa baraza kuu la Chadema ambapo utakuwa mkutano mkubwa na wa aina yake.
Akizungumzia masuala ya maandalizi Mbassa amesema kwa sasa maandalizi yanaendelea vizuri na kila kamati iliyopewa majukumu yake inaendelea kuyatekeleza.
Aidha mkutano huo mkuu wa baraza la Chadema Taifa unatarajia kuwa na wajumbe wa baraza kuu na kamati kuu pamoja na wasiokuwa wajumbe wafikao 1,500.
Amesema mpaka sasa kamati ya mapokezi imeisha tafuta nyumba za kutosha za kulaza wageni huku suala la chakula na vinywaji kwa wageni pamoja na watu mbalimbali maandalizi yakiwa yamekamilika.
Kuhusu ulinzi amesema kwa sasa ulinzi katika mkoa wa Dodoma kwa kupitia walinzi wake wa chama (Red Brigade) wamejipanga vizuri, ikiwa ni pamoja na ulinzi wa jeshi la polisi kwa maana ya kuwa tayari wameisha pewa taarifa ya ujio wa baraza hilo.
Naye Makamu Mwenyekiti, Aisha Yusufu amesema maandalizi ya kutundika bendera za chama yamekamilika na wapo vijana wa kutosha ambayo watatundika bendela hizo kuanzia kesho.
Aidha amesema katika baraza hilo kutakuwepo na viongozi marafiki wa chama hicho kutoka nchi za nje ambao watahudhuria baraza kuu kwa lengo la kushuhudia jinsi demokrasia ndani ya Chadema inavyotekelezwa.
Amesema maandalizi ya baraza kuu yanaandariwa na uongozi wa kanda ya kati na maandalizi hayo kwa sasa yamefikia hatua nzuri nay a kuridhisha.
Leave a comment