CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na ACT-Wazalendo vimeomba kuitishwa upya Uchaguzi Mkuu wa Urais, wabunge, wawakilishi na madiwani, kwa maelezo kwamba havikubaliani na matokeo ya Uchaguzi wa tarehe 28 Oktoba, 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tamko la msimamo limetolewa leo tarehe 31 Oktoba, 2020 jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.
“Kwa umoja wetu tunaamini kilichofanyika katika uchaguzi wa tarehe 28 Oktoba, 2020 hakina sifa wala uhalali wa kuitwa Uchaguzi Mkuu bali ni unyang’anyi na uporaji wa kutumia nguvu dhidi ya haki ya Watanzania kuchagua viongozi wanaowataka,” amesema Mbowe.
Aidha, Mbowe amesema vyama hivyo vinaagiza Tume ya Taifa ya Uchaguzi Tanzania (NEC) na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), kuvunjwa na kuundwa tume huru itakayosimamia uchaguzi huo.
“Tunadai kuitishwa upya kwa Uchaguzi Mkuu haraka iwezekanavyo. Tunahitaji kuvunjwa ZEC na NEC kuundwa tume huru ya uchaguzi itakayosimamia uchaguzi huo,” amesema Mbowe.
Kwa upande wake Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe amesema chama chake kinaunga mkono msimamo huo, na kuwaomba Watanzania kuchukua hatua kupinga matokeo ya uchaguzi huo.
Aliyekuwa Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chadema, Tundu Lissu amesema “Mimi nawataka wananchi wetu wachukue mamlaka yao tena. Kuhakikisha hayo matokeo ya uchaguzi yanabadilishwa ili tuwe na uchaguzi wa kutoa mamlaka kutoka kwa wananchi kwenda kwa wawakilishi wao mbalimbali.”
Pamoja sana