CHAMA tawala nchini Tanzania- Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeteua majina mawili ya wanachama wake, watakaogombea Uspika na Naibu Spika wa Bunge la 12 la Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Pia, chama hicho, kimeteua jina moja la mwanachama wa chama hicho kuwania Uspika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
Uteuzi huo umefanywa na kikao cha kamati kuu ya CCM kilichokutana juzi Alhamisi jijini Dodoma tarehe 5 Novemba 2020 chini ya Mwenyekiti wa chama hicho, Rais John Magufuli.
Walioteuliwa ni; Job Ndugai kuwa mgombea Uspika na Dk. Tulia Ackosn kugombea Naibu Spika wa Bunge la Tanzania.
Katika Bunge la 11 lililomaliza muda wake, Ndugai ambaye ni mbunge mteule wa Kongwa alikuwa Spika huku Dk. Tulia ambaye naye ni mbunge mteule wa Mbeya Mjini alikuwa Naibu Spika.
Kupitishwa wao pekee ina maana, wanakwenda kutetea nafasi hizo huku kukiwa na uwezekano mkubwa wa kushinda kutokana na wingi wa wabunge wa CCM.
Pia, kikao hicho, kimemteua, Zubeir Ali Maulid kuwa mgombea Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
Kama ilivyo kwa Ndugai na Dk. Tulia, naye Maulid alikuwa Spika wa Baraza la Wawakilishi lililomaliza muda wake ambaye anakwenda kutetea nafasi hiyo.
Leave a comment