Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa CCM ‘yawagwaya’ Chenge, Muhongo, Ngeleja
Habari za SiasaTangulizi

CCM ‘yawagwaya’ Chenge, Muhongo, Ngeleja

Spread the love

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimesema kwa sasa hakiwezi kuwachukulia hatua wabunge wa chama hicho ambao wamekuwa wakihusika mara kwa mara katika kashfa za ufisadi, anaandika Hamis Mguta.

Humphrey Polepole, Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), anayeshughulikia Itikadi na Uenezi amewambia wanahabari leo Lumumba, jijini Dar es Salaam kuwa hawawezi kuchukua hatua kwa wanachama hao mpaka pale itakapoonekana ni tishio kwa ustawi wa chama hicho.

Andrew Chenge Mbunge wa Bariadi, William Ngeleja, Mbunge wa Sengerema na Profesa Sospeter Muhongo – wote CCM, wamekuwa wakitajwa kuhusika katika kashfa za ufisadi mara kwa mara, ilitarajiwa kuwa CCM ingetangaza kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya wabunge hao.

“Sisi kama chama tunasubiri matokeo ya vyombo vya uchunguzi na ikionekana kwamba watu hawa hawana tatizo tutawaacha lakini ikionekana wana shida inayoteteresha taswira ya CCM kwa umma, chama hakitakuwa na ajizi,” amesema Polepole.

Ngeleja, Chenge na Muhongo walihusika katika kashfa ya mabilioni ya fedha za Escrow mwaka 2014 iliyosababisha kupanguliwa kwa Baraza la Mawaziri, lakini pia wabunge hao wote wametajwa kuhusika katika kashfa ya wizi wa dhahabu kupitia mchanga wa dhahabu (makinikia).

Chenge pia amewahi kutajwa kuhusika katika kashfa ya mabilioni ya ununuzi wa rada. Huku akituhumiwa kuhifadhi zaidi ya Sh. 1.2 bilioni katika kisiwa cha New Jersey Marekani, hata hivyo hajawahi kushtakiwa mahakamani wala kuchukuliwa hatua na chama chake.

Polepole amewaeleza wanahabari kuwa, ni huenda hatua zikachukuliwa dhidi ya wanachama walioshiriki katika kashfa za ufisadi hata hivyo, hakueleza ni hatua zipi za kinidhamu zinazoweza kuchukuliwa dhidi ya wanachama hao akiwemo Chenge, Ngeleja na Prof. Muhongo.

Ameeleza kuwa makada wote wa chama hicho waliotuhumiwa kujihusisha na mikiataba ya madini iliyolitia hasara taifa wanatakiwa kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola ili ndipo CCM iweze kuangalia hatua za kuchukua.

Polepole amesema kuwa kanuni za maadili ya viongozi za CCM haziruhusu viongozi wa chama hicho kujihusisha na ufisadi, wizi na kupokea rushwa, na kwamba wataangalia hatua za kuchukua iwapo wabunge hao watathibitika kufanya vitendo vya hujuma,

“Tunahangaika kuurekebisha na kuuondoa mfumo mbaya ndani ya chama chetu, tunatambua kulikuwa na makosa na ndiyo maana tunayarekebisha waziwazi kwa maslahi ya watanzania,” amesema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

error: Content is protected !!