MCHAKATO wa kura za maoni za kuwatafuta wagombea udiwani, ubunge na uwakilishi wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kufanyika kwa uwazi. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na CCM, Mikutano Mikuu ya CCM ya Wilaya kwa ajili ya kupiga kura za maoni za wagombea ubunge na udiwani, itafanyika tarehe 20 hadi 21 Julai 2020.
Baada ya hatua hiyo, tarehe 30 Julai 2020, vikao vya kamati za siasa za jimbo, vitafanyika kuwajadili wagombea na kutoa mapendekezo yake kwa kamati za siasa za wilaya, ambayo itafanya vikao vyake tarehe 1 hadi 2 Agosti 2020.
Tarehe 4 hadi 5 Agosti 2020, vikao vya kamati za siasa za mkoa vitafanyika kuwajadili wagombea na kutoa mapendekezo yake kwa kamati kuu ya halmashauri kuu ya CCM (NEC).
Akizungumza katika mkutano wa kueleza utekelezaji wa Ilani ya CCM mkoani Ruvuma, leo Jumamosi tarehe 18 Julai 2020, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole amesema, michakato hiyo itafanyika kwa uwazi ikiwa ni
utekelezaji wa azma ya Rais John Magufuli, Mwenyekiti wa chama hicho, ya kuhakikisha uteuzi wa wagombea unafanyika kwa uwazi.
Katika mikutano yake miwili ya CCM iliyofanyika tarehe 10 na 11 Julai 2020 jijini Dodoma, Mweneykiti wa CCM, Rais Magufuli alitoa maagizo iwe wazi na waandishi wa habari kuruhusiwa kuhudhuria ikiwemi kuirusha moja kwa moja.
“Mweneyekiti wa CCM ametuonesha mfano, ambao umetengeneza desturi mpya tutakayoishi nayo muda mrefu, awali ilikuwa ni desturi wajumbe wa halmashauri kuu tunajifungia ndani, tutajadili kisha tutapiga kura.”
Soma zaidi hapa
JPM: Sijamtuma mtu akagombee, awapa ujumbe wanaCCM
“Kipindi hiki, Rais Magufuli alisema hakuna kuingia ndani hapana, tunapiga kura hapahapa na wanahabari msiwaambie tokeni,” amesema Polepole.
Aidha, Polepole amesema wenyeviti wa mashina maarufu kama mabalozi, watashiriki katika kura za maoni za kupitisha wagombea udiwani.
Polepole amewaagiza viongozi wa CCM wa wilaya, kuhakikisha mabalozi wanashiriki kwenye michakato hiyo.
“Kwa mara ya kwanza, wenyeviti wa mashina katika kata husika, mabalozi ndio kiungo muhimu cha chama na umma, tumesema nani anafaa kwa nafasi ya udiwani kwenye kata, hilii ni wenyeviti wetu wa mashina wanajua, “ amesema Polepole.
Hatua ya mabalozi kushiriki katika michakato ya utafutaji wagombea udiwani wa CCM, imekuja baada ya Katiba ya CCM kufanyiwa marekebisho, yanayoruhusu mabalozi kushiriki kwenye mikutano mikuu ya kata na wadi, ili kupiga kura ya wagombea wa nafasi hizo.
Katiba ya CCM ilifanyiwa marekebisho katika Mkutano Mkuu wa chama hicho, uliofanyika tarehe 11 Julai 2020, jijini Dodoma.
Leave a comment