MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania, Rais John Pombe Magufuli, amependekeza kampeni za Uchaguzi Mkuu utakaofanyika tarehe 28 Oktoba 2020 za chama hicho, zizinduliwe jijini Dodoma. Anaripoti Mwandishi Wetu…(Dodoma)
Ratiba iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) inaonyesha kampeni za Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020, zitaanza 26 Agosti hadi 27 Oktoba 2020.
Dk. Magufuli ambaye ni Rais wa Tanzania ametoa pendekezo hilo leo Alhamisi tarehe 6 Agosti 2020 makao makuu ya chama hicho, mara baada ya kutoka Ofisi za NEC jijini Dodoma kuchukua fomu za kuwania Urais wan chi hiyo.
Akizungumza na mamia ya wanachama waliojitokeza ofisini hapo, Rais Magufuli amesema, “ninawaomba viongozi wenzangu kuzindua kampeni hizi ikiwezekana tuanzie Dodoma sababu ndio makao makuu ya nchi.”
Hata hivyo, Rais Magufuli, hakupendekeza tarehe ya uzinduzi huo wa kampeni.
Amesema, chama hicho kimeandaa Ilani ya Uchaguzi ya CCM nzuri na yenye mambo mengi yenye tija kwa Watanzania wote bila kujali kidini, kabila au itikadi za kisiasa.
“Ilani ya CCM tayari imekamilika, kitabu hiki hapa ambacho mtakinadi, mnaweza kukiona kitabu cha mwaka huu ni kikubwa sana kuliko cha miaka mitano iliyopita, maana yake kina mambo mengi sana, siwezi kuyasema hapa tutasema siku ya uzinduzi wa kampeni,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli alisindikizwa na mgombea mwenza, Samia Suluhu Hassan na viongozi mbalimbali wa chama hicho akiwemo, Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa CCM pamoja na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Leave a comment