CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Kagera kimedhamiria kuwavua madaraka viongozi ambao wataonekana kuwavuruga wakati huu kuelekea chaguzi zijazo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizumgumza katika semina ya kujenga chama hicho Wilaya ya Bukoba vijijini, Mwenyekiti wa CCM mkoani Kagera, Costansia Buhiye amesema kuwa, watu hao ni kama mamluki na kuwa, lazima wahakikishe wanawatimua au kuwavua wadhifa pindi watakapobaini.
“Kuna mamluki bado ndani ya CCM, na wengine viongozi na watendaji wa chama. Kwa hivi sasa tumejipanga kuwaondoa kwa njia yoyote na hawafanyi kazi ambayo walipewa. Kazi yao kubwa ni kukifitinisha chama na wanachi wake,” ameeleza Buhiye.
Ameongeza kuwa, chama hiki inabidi wanachama wake kujenga mshikamano na wananchi hata wa vyama vingine, ili waweze kukichagua chama hiki katika chaguzi zijazo.
Amesema, malumbano na vitu ambavyo sio vya msingi ikiwemo kupitisha watu wasikubalika, ndio vilipelekea chama hicho kupoteza baadhi ya mitaa, kata na majimbo kwenye chaguzi za nyuma.
Mbunge wa Jimbo la Bukoba vijijini, Jasson Rweikiza amesema kuwa, semina hiyo ni muhimu katika kuwajenga wanachama kiuongozi na kiutawala.
Amesema kuwa, wanachama wafuate misingi ya chama na kuacha kuanza siasa za uchaguzi na kuwa, muda bado na wakifanya hivyo wanakuwa wamekiuka Katiba ya chama chao.
Leave a comment