SERIKALI inatakiwa kuchukua hatua dhidi ya wanasiasa wakiwemo wale waliostaafu ambao wameshindwa kurejesha mikopo ya matrekta waliyopata kutoka Shirika la Uzalishaji Mali linaloendeshwa na Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT). Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Agizo hilo limetolewa bungeni na mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Naghenjwa Kaboyoka wakati akiwasilisha taarifa ya kazi za kamati hiyo kwa mwaka wa 2018.
Kaboyoka ambaye ni mbunge kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), alisema kuna limbikizo kubwa la deni linalotokana na hatua ya kutorejeshwa mikopo ambayo kwa sehemu kubwa walionufaika ni wanasiasa.
Wanufaikaji wengine wa mikopo hiyo iliyofikia thamani ya Sh. Bilioni 40 na ambayo ilianza kutolewa mwaka 2011 mpaka 2016, ni taasisi mbalimbali. Taarifa ya Kaboyoka ilisema deni hilo ni la kufikia Juni 30 mwaka 2017.
Alisema uchambuzi wa kamati umebaini kuwa baadhi ya wadaiwa sugu wa mikopo ni viongozi katika serikali wa sasa na waliostaafu.
“Kama jitihada za dhati hazitafanyika kuna viashiria kuwa madeni hayo hayatalipwa na kuiweka Suma JKT katika hali ngumu kiutendaji… kutorejesha mikopo ni ukiukaji wa mikataba na ni kuisababishia hasara serikali,” alisema.
Ndipo alipotoa kauli kwamba, “… Bunge linaazimia kwamba serikali ifanye uchunguzi wa kina ili kubaini taratibu zilizotumika katika utoaji wa mikopo ya matrekta kwa watu na taasisi mbalimbali na ichukue hatua stahiki kwa wahusika wanaodaiwa.”
Leave a comment