Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Bunge, Serikali wasaka siri za Tundu Lissu
Habari za SiasaTangulizi

Bunge, Serikali wasaka siri za Tundu Lissu

Spread the love

USIRI uliotanda kuhusu matibabu ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Antipas Lissu, anayetibiwa nchini Kenya, unaitesa serikali na uongozi wa Bunge la Tanzania, anaandika Mwandishi Wetu.

Taarifa kutoka vyanzo vyetu mbalimbali zinasema, wakuu wa Bunge na Serikali, mihimili ya dola, wamekuwa wakihaha kutafuta taarifa za kinachoendelea kwenye matibabu ya mwanasiasa huyo na kiongozi mwandamizi katika Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Lissu alijeruhiwa kwa kumiminiwa risasi zaidi ya 30 mwilini katika shambulio lililofanywa Septemba 7 mwaka huu akiwa mjini Dodoma kwa shughuli za Bunge. Tangu hapo, amekuwa akitibiwa katika Hospitali ya Nairobi (Nairobi Hospital) nchini Kenya.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, kutokana na kuwapo usiri mkubwa, Bunge liliamua kuitisha kikao maalum na familia ya Lissu ili kupata mwanya wa kufahamu kinachoendelea kuhusu matibabu ya mbunge huyo.

Kikao cha familia ya Lissu na Bunge, kilifanyika Jumatatu wiki hii, kwenye ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Spika Job Ndugai, Naibu wake, Dk. Tulia Ackson, Mbunge wa Vunjo, James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Mbunge wa Hanang, Mary Nagu (CCM).

Wengine waliohudhuria kikao hicho, ni Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashilillah, Katibu wa Spika, Said Yakoub, Alute Mughwai ambaye ni kaka mkubwa wa Lissu, dada yao mkubwa na mdogo wao aitwae Vicenti.

Lissu ambaye pia ni Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani na Mwanasheria wa Chadema, alishambuliwa nje ya nyumba yake eneo la Area D, mjini Dodoma alipowasili akitokea bungeni baada ya kumaliza kipindi cha asubuhi.

MwanaHALISI Online limefahamishwa na vyanzo vya habari kuwa “usiri uliotawala matibabu ya Lissu, umesukuma uongozi wa Bunge kuitisha kikao cha wanafamilia.”

“Bunge na hata serikali wanahaha kupata taarifa za matibabu ya Lissu… ni matokeo ya bunge kujiweka pembeni na jambo hili tokea mwanzo,”

Anasema mtoa taarifa. “Siyo spika wa Bunge wala serikali anayejua Lissu ameumia vipi na anatibiwa sehemu gani ya mwili wake. Hawajui matibabu yake yatachukua muda gani na ni nani hasa anayelipa gharama zake.”

Kutokana na hali hiyo, na kwa kuwa chama chake kimeamua kuchukua dhamana kuhusu matibabu ya Lissu katika msingi wa kuwa jukumu la kusimamia matibabu ni la kifamilia zaidi, Bunge limejikuta gizani.

“Bunge liliyumba tokea awali… sasa linajaribu kujirejesha kwa nguvu kupitia familia. Lakini mpango huu hauwezi kufanikiwa kwa kuwa familia ya Lissu imebaki na msimamo wa kutopokea fedha kutoka serikalini,” ameeleza mtoa taarifa.

Taarifa ndani ya kikao kati ya uongozi wa Bunge na familia zinasema mkakati wa Bunge kujiweka karibu na Lissu umepata mtihani. Ni kutokana na familia kukataa kutoa taarifa iwapo Chadema haikuwakilishwa kikaoni.

“Chadema haikuhudhuria kikao kile. Sasa familia imegoma kuridhia matakwa ya Bunge,” anaeleza.

Taarifa zinasema mbele ya kikao, Bunge liliwasilisha pendekezo la kutaka kuwa mratibu na mlipaji mkuu wa matibabu ya Lissu. Familia imekataa.

Mmoja wa wanafamilia alinukuliwa akikiambia kikao hicho kwamba wapewe muda wa kujadiliana kuhusu mapendekezo ya Bunge. Wa kujadiliana nao ni uongozi wa juu wa Chadema.

“Kutokana na utata uliogubika na serikali inavyoshambuliwa kwa kushindwa kukamata watuhumiwa, hatuwezi kuridhia lolote hapa,” alinukuliwa mwanafamilia akisema kikaoni.

Familia ya Lissu, kwa mujibu wa taarifa hizo, imeomba muda w amashauriano kwa kuwa imekuwa ndio msimamo wa Lissu mwenyewe kitandani, “niko tayari kufa kuliko kutibiwa kwa masharti.”

Kikao cha familia ya Lissu na uongozi wa Bunge kilifanyika Jumatatu jijini Dar es Salaam kuanzia saa 3:55 asubuhi mpaka saa 7:40 mchana.

Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, amekiri kutofikiwa kwa muafaka katika kikao hicho kuhusu mapendekezo ya Bunge.

“Ni kweli tulikutana na kuzungumza na familia ya Lissu, lakini hatukuweza kufikia mwafaka kutokana na msimamo wa familia. Tumekubaliana kukutana tena wakati mwingine,” alisema.

Alipoulizwa ni kipi kimesababisha mkwamo, Mbatia alisema, “ni kutoaminiana.” Upande wa Chadema na familia umeonekana kutokubaliana kuhusu msimamo wa Bunge. Kauli za Bunge na zile za Ummy Mwalimu, zimechangia kwa kiwango kikubwa kuwepo ufa wa mahusiano kati ya pande hizi mbili.”

Ummy ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii jinsia Wazee na Watoto,  ambaye wiki iliyopita alisikika akitoa msimamo wa serikali kuwa ipo tayari kugharamia matibabu ya Lissu kokote nje ya nchi. Awali, waziri huyo na bunge walinukuliwa wakisema mjini Dodoma kuwa serikali imejiondoa kwenye suala hilo baada ya familia ya Lissu kushikilia kumchukua na kumpatia matibabu nje ya nchi.

Akizungumzia kikao cha familia na Bunge, Alute, kaka wa Lissu, alikiri kutokamilika kwa mazungumzo. Sababu ameitaja kuwa ni kukosekana kiongozi kutoka Chadema.

Alute ambaye kama Lissu, naye ni wakili wa Mahakama Kuu, anayefanyia shughuli zake mkoani Arusha, alisema, “siwezi kusema zaidi ya hayo.”

Anasema, “moja ya masharti tuliyopeana ni kutokusema hadharani, mambo tuliyoyajadili yanamuhusu Lissu.”

Hakuna kiongozi aliyekuwa tayari kueleza sababu za Chadema kukosa uwakilishi kwenye kikao hicho.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

error: Content is protected !!