BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, limepitisha azimio la kuitaka Serikali kutobadili uamuzi wa Jiji la Dodoma kuwa makao makuu ya nchi na shughuli zake. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Azimio hilo limewasilishwa leo Jumatatu tarehe 8 Juni 2020, na Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM).
Akisoma taarifa ya azimio hilo, Mabula amesema Bunge limefikia hatua hiyo kutokana na makao makuu kuwa Dodoma, ni takwa la wananchi wengi, mkoa huo upo katika eneo la kimkakati kwa masuala ya ulinzi na usalama.
“Dodoma ipo katikati ya nchi na mikoa mingine Kijiografia, inawezesha huduma kusogezwa karibu na wananchi na hivyo kurahisisha utawanyaji wa maendeleo nchini.”
“Na vilevile makao makuu kuwa Dodoma kunaleta ufanisi na tija katika uendeshaji wa shughuli za Serikali na kupunguza gharama za uendeshaji,” amesema Mabula wakati akisoma azimio hilo bungeni.
Kufuatia azimio hilo, Mabula amesema, Bunge linaitaka Serikali, mamlaka au mtu yeyote kutotengua uamuzi wa wananchi wa kuifanya Dodoma kuwa makao makuu ya nchi.
“Bunge limeazimia kuitaka Serikali na taasisi zake kutohamisha kwa namna yoyote shughuli za Serikali kutoka Dodoma kwenda sehemu nyingine yoyote ya nchi,” amesema Mabula.
Wakati huo huo, Mabula amesema Bunge limeitaka Serikali kuhakikisha, inaendelea kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya kuboresha na kuendeleza miundombinu ya Jiji la Dodoma wakati wote, ili kuwa na mandhari yanayoendana na hadi ya makao makuu ya nchi na Serikali.
Julai mwaka 2016, Rais John Magufuli alitoa amri kwa wizara, mamlaka na taasisi za serikali kuhamishia ofisi zao mkoani Dodoma.
Amri hiyo ilianza kutekelezwa kwa wizara kadhaa kuhamia, ambapo Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu, alihamia rasmi Dodoma tarehe 26 Septemba 2016, huku Rais Magufuli akihamia rasmi mwishoni mwa mwaka 2019.
Leave a comment