ALHAJI Abdallah Bulembo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), ametangaza kung’atuka rasmi katika nafasi yake, kwa mdai kuwa anahitaji kuumzika, anaandika Dany Tibson.
Bulembo ambaye hivi karibuni ameteuliwa kuwa Mbunge na Rais John Magufuli amesema hana mpango wa kugombea nafasi yoyote ndani ya CCM katika uchaguzi mkuu wa chama hicho unaofanyika mwaka huu.
Ametoa kauli hiyo katika baraza la dharura la jumuiya ya wazazi wa CCM kilichohudhuriwa na wajumbe 102.
“Si kwamba sina uwezo wa kugombea tena, ila tu nimeamua kupumzika na nikatulie kijiji kwangu huku nikiendeleza shughuli nyingine.
“Msidhani kwamba nang’atuka kutokana na ubunge niliochaguliwa. Hapana, mimi ni mbunge ambaye jimbo langu ni Ikulu,” amesema.
Amesema ni wakati wa wajumbe wengine kutoka ndani ya jumuiya hiyo kuchangamkia fursa ya kugombea nafasi hiyo ya uwenyekiti bila kutegemea kubebwa na mtu yoyote.
“Msitegemee kuwa nitampigia mtu kampeni, nendeni mkachukue fomu ya kugombea kama mmejipima na kuona mna uwezo na asije mtu yoyote akasikika huko akiwadanganya kuwa ameongea na mimi na kwamba nitamuunga mkono katika uchaguzi,” amesisitiza.
Bulembo amedai kuwa mwanzoni Jumuiya ya wazazi ya CCM ilikuwa na wakati mgumu lakini yeye kama mwenyekiti kwa kushirikiana na viongozi wengine waliamua kufanya kazi ya kuiweka mahali mazuri jumuiya hiyo.
Leave a comment