Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Bulaya amvaa tena Rais Magufuli, amwambia hajamaliza kazi
Habari za SiasaTangulizi

Bulaya amvaa tena Rais Magufuli, amwambia hajamaliza kazi

Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini
Spread the love

BAADA Ya Rais John Magufuli kufuta kanuni mpya ya kikokotoo cha mafao ya watumishi wa umma iliyotokana na Sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma Na. 2 ya mwaka 2018, Chama cha Chadema kimetoa wito kwa serikali kurudisha bungeni kwa hati ya dharula sheria hiyo, kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).

Akizungumza na wanahabari leo tarehe 2 Januari 2019 jijini Dar es Salaam, Waziri Kivuli wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana na Walemavu, Ester Bulaya amesema tiba ya mapungufu yaliyomo katika sheria hiyo, ni kurudishwa bungeni kwa ajili ya maboresho, ili hata agizo la Rais Magufuli la kufuta kikokotoo hicho liweze kutekelezeka kwa mujibu wa sheria.

Bulaya ameeleza kuwa, suala la kumpa mamlaka waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi kutunga kanuni hiyo, lipo kwenye sheria, na kwamba ili kanuni hiyo ibatilishwe, inabidi Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) ahakikishe sheria husika inarudi bungeni kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho.

“Sasa kama lipo kwenye sheria lazima liende likabatilishwe bungeni na hii ni kazi ya bunge, isiishie tu tamko la rais. Hili ni jambo la msingi, ikiishia hivi hili jambo halitatkelezeka, lazima lirudi bungeni ili liweze kufanyiwa kazi,” amesema na kuongeza Bulaya.

“Sheria ambayo tumetoka kuipitisha bungeni ambayo kuna mambo kadha wa kadha tulipinga. Tiba yake ni kurudishwa bungeni kwa hati ya dharula ili haya mambo yawe kisheria. Tunaenda kwenye kamati hivi karibuni AG aanze kuchukua maoni ya wadau sababu bila hivi haya mambo hayatatekelezeka kisheria. Isiishie kwenye kauli tu, iletwe bungeni ili haya mambo yawe kisheria katika hiki kipindi cha mpito.”

Vile vile, Bulaya amesema sheria hiyo inabidi ifanyiwe marekebisho ili kuondoa sintofahamu kuhusu suala la fao la kujitoa ambapo wafanyakazi wanaopoteza ajira zao, sheria hiyo inawakataza kupata mafao yao kwa wakati husika.

“Lakini kuna mambo mengi, sio hiyo asilimia 50 wala sio la kikokotoo, tumeona kuna suala zima la fao la kujitoa, na ninyi mnajua hili jambo limezua mtafaruku mkubwa na tulisemea katika kikao kilichopita, na rais nae alilisemea na suala hili liko kisheria na sheria imekataza, ili kufanikisha hili jambo sheria irudi bungeni liondolewe.

Kwanza mnajua hali halisi ya sasa hivi ya maisha ikoje, hali ya kibiashara ilivyo mbaya, waajiri wanafukuza wafanyakazi kila siku, lakini kuna sheria inafanya kazi inazuia yule mtu aliyefukuzwa kazi asitoe fedha zake. Hili jambo halitakiwi kuishia kama tamko tu la rais, lazima iletwe bungeni kwa hati ya dharula, ili na yale rais anakubaliana nayo yasiishie maneno, yakiishsia maneno tutaona ni siasa ya kutafuta kura 2020 na baada ya hapo wafanyakazi wanataabika.” Amesema.

Bulaya amesema suala lingine ambalo linatakiwa kufanyiwa marekebisho ni nafasi za uwakilishi wa watumishi wa umma katika Bodi ya Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSSSF).

“Uchache wa wajumbe wa bodi, uwakilishi wa wafanyakazi ni mdogo inapokuja sula la kufanya maamuzi kwenye suala linalohusu wafanyakazi wanamezwa, kisheria lipo wamepewa wawakilishi wawili, ndio maana tunasema hapana kuishia kwenye kauli, lazima tumtake AG alete bungeni ili sisi tunaona inafaa kuwe na wawakilishi wa kutosha kwenye bodi ili waweze kusimamia haki zao kama watumishi,” ameshauri Bulaya.

Katika hatua nyingine, Bulaya ameitaka serikali kuwalipa fidia wastaafu waliolipwa mafao yao kwa kutumia kikokotoo kilichofutwa na Rais Magufuli

“Baada ya kanuni hiyo kutekelezwa kuna watu walipunjwa pesa zao, hawa wote wanapaswa kufidiwa kile kiasi kilichobaki, sababu ya kanuni hizi zilipoanza kutekelezwa mwezi wa nane walipata fedha pungufu, hivyo wanaopaswa kupata fedha zao zote kama kweli kuna dhamira na kama jambo hili halijafanyika kisiasa ili kupisha uchaguzi wa serikali za mitaa wa 2019 na uchaguzi mkuu 2020 inapaswa walipwe fedha zao,” amesema Bulaya.

Hali kadhalika, Bulaya ameitaka serikali kulipa madeni inayodaiwa na mifuko ya hifadhi ya jamii ili kuiwezesha mifuko hiyo kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Chadema: Samia aunde tume kuchunguza mauaji mgodi wa Barick

Spread the loveRAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameombwa aunde tume huru kwa...

KimataifaTangulizi

Zuma akataliwa kugombea urais

Spread the love  TUME Huru ya Uchaguzi Afrika Kusini (IEC) imemwondoa rais...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

error: Content is protected !!