ESTER Bulaya, Mbunge wa Tarime Mjini ambaye ni mshtakiwa wa tisa, kwenye kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi tisa wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa mawazo ya wabunge wa upinzani hayazingatiwi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Bulaya kwenye kesi hiyo namba 112 ya mwaka 2018, ameshtakiwa pamoja na Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema-Taifa, Vicent Mashinji, Katibu Mkuu Chadema-Taifa, Salum Mwalim, Naibu Katibu Mkuu, Chadema-Zanzibar, John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu Chadema-Bara.
Wengine ni John Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, Mch. Peter Msigwa, Mbunge wa Iringa Mjini, Ester Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini na Halima Mdee, Mbunge wa Kawe.
Leo tarehe 5 Desemba 2019, Bulaya, ameanza kutoa utetezi wake mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba akiongozwa na wakili wa utetezi Peter Kibatala.
Bulaya ameulizwa na Kibatala juu ya namna wabunge wa upinzani wanaweza kushiriki kwenye kutunga sheria ndiyo alipojibu kuwa wabunge wa upinzani wakitoa maoni yao, hayazingatiwi kwa kuwa wabunge wa upinzani wachache bungeni.
Aliulizwa kuhusu sheria zilizopita bila mchango wa mawazo yao, aliainisha sheria ya Vyama vya Siasa, sheria ya Mfuko wa hifadhi ya jamii na Sheria ya makosa ya mtandao.
Bulaya ameieleza mahakama kuwa, kuanzia tarehe 1 Februari hadi tarehe 11 Februari mwaka huu, alikuwa Dodoma na tarehe 11 hadi 15 Februari, alikuwa jimboni kwake Bunda na kwamba usiku wa tarehe 15 alisafiri kwa ndege hadi Dar es Salaam.
Bulaya ameieleza Mahakama kuwa alikuja Dar es Salaam kwa lengo la kuhudhuria ufungaji wa mkutano wa kampeni za mgombea ubunge katika uchaguzi mdogo wa jimbo la Kinondoni.
Amedai kuwa alifika kwenye mkutano huo majira ya saa tisa alasiri, na aliondoka majira ya saa 11 ambapo aliondoka na Halima Mdee aliyekuwa akiumwa, ambaye siku ya pili alimsindikiza kwenye hospitali ya St. Parrot jijini CapeTown, Afrika Kusini kwa matibabu.
Bulaya ameeleza Mdee alitibiwa kwa takribani wiki mbili na siku waliyorudi nchini, Mdee alitiwa mbaroni na jeshi la Polisi ilhali yeye hajakamatwa.
Bulaya ameeleza kuwa ameitwa na jeshi la Polisi mwezi mmoja baadaye tangu siku aliyokamatwa Mdee.
Kesho saa 4 na nusu upande wa mashtaka utamhoji shahidi huyo.
Leave a comment