ABIRIA zaidi ya 50 waliokuwa wakitarajia kusafiria na ndege ya Bombidier jijini Mwanza, wameshindwa kusafiri kutokana na ubovu wa ndege hiyo kitendo kilichosababisha abiria wengi kulalamika, anaandika Moses Mseti.
Hiyo ni mara ya tatu kwa ndege hizo mbili zilizoanza kufanya kazi katika awamu ya Rais John Magufuli zikipata hitilafu ya kiufundi kwani, miezi mitatu iliyopita ndege moja, iliibua taharuki kubwa uwanjani hapo.
Mwaka jana wakati ndege hizo zikipokelewa jijini Dar es Salaam, serikali iliwahakikishia Watanzania kwamba ni mpya na zilitoka kiwandani moja kwa moja.
Hata hivyo baadhi ya wanasaiasa walinukuliwa wakisema ndege hizo hazikuwa mpya na kwamba hazina hata mwendo.
Ndege hiyo ambayo ni mali ya serikali, ilishindwa kuruka zaidi ya mara mbili kutokana na hitilafu ya kiufundi kwenye injini hatua ambayo ilisababisha abiria waliokuwa wakitarajiwa kusafiri kushushwa.
Ndege hiyo ilitarajiwa kuondoka saa mbili na nusu asubuhi kutoka uwanja wa ndege wa Mwanza kwenda mjini Bukoba.
Mmoja wa abiria waliokuwa kwenye ndege hiyo, aliyeomba jina lake kuhifadhiwa, amedai walitarajiwa kuondoka na ndege hiyo saa mbili na nusu asubuhi lakini ilishindikana.
Amesema kukwama kwa ndege hiyo kutasababisha kazi zake alizotarajiwa kuzifanya mkoani Kagera kusimama huku akidai mpaka muda huo hawajaelezwa tatizo linalosababisha ndege hizo kupata hitilafu.
“Leo majira ya asubuhi abiria waliofika uwanjani hapo kwa ajili ya safari zao, lakini cha kusikitisha baada ya kupewa taarifa hakutakuwepo na safari, walianza mvutano na uongozi uliodumu kwa saa tatu,” amsema
Mtoa taarifa huyo amesema kuwa, ndege hizo za serikali zinazokuwa zinapata hitilafu ya mara kwa mara kutasababisha wakose imani na nazo na kuiomba serikali kuchukua hatua kuhakikisha zinatoa huduma bila hofu.
“Nilipofika hapa asubuhi kwa ajili ya safari, tukaambiwa ndege imepata hitilafu na mpaka muda huu (saa nane) mchana bado tunasubiri tunadanganyishiwa chakula tu na mambo yetu mengi yamekwama,” amesema,” amesema
Meneja wa uwanja wa ndege wa Mwanza, Easter Madale, alipotafutwa kuzungumzia suala hilo kupitia simu yake ya mkononi, alidai yupo kikazi mkoani Tabora huku akidai kuwa utafutwe uongozi wa ATC.
Meneja wa Shirika la Ndege Tanzania (ATC) mkoani Mwanza, Theonestina Ndyetabula, alipotafutwa na mtandao huu saa sita mchana kupitia simu yake ya mkononi, alidai hawezi kuzungumza kwa wakati huo na kwamba kuna mambo anayashughulikia.
Ndyetabula, pia alipotafutwa kwa mara nyingine tena saa 7:36 mchana, alisema,” bado yupo bize kuna jambo analishughulikia,” amesema na kukata simu yake.
Mpaka mchana huu, abiria hao waliotarajia kusafiri kuelekea mkoani Kagera bado walikuwa Mwanza huku mmoja wa wafanyakazi wa ATC akinukuliwa akisema hakuna uwezekano wa abiria hao kusafari.
Mpaka sasa tatizo lililosababisha ndege hiyo kushindwa kufanya safari zake, haijafahamika licha ya taarifa zisizokuwa za uhakika kudai kwamba kuna tatizo kwenye injini ya kushoto.
Leave a comment