BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini (HESLB), imetangaza vita dhidi ya waajiri hapa nchini ikiwamo wale wa serikali ili kubaini mishahara wanavyolipwa wafanyakazi na kiasi wanachowakata na kukiwasilisha kwao kulipia deni la elimu ya juu kila mwezi. Anaandika Hamis Mguta…(endelea).
Wafanyakazi mbalimbali hapa nchini ambao walichukua mkopo kutoka HESLB kwa ajili ya kugharamia elimu ya juu wanatakiwa kukatwa deni kutoka kwa waajiri wao na kuwasilisha fedha hizo kwa bodi.
Msako huo ambao utagusa sekta binafsi na serikali unatarajia kuanza Januari 8, 2017 na kukagua taarifa za mishahara za waajiri (payroll) ili kubaini waajiri ambao wanawasilisha kiwango kidogo cha mikopo ya wafanyakazi wao.
Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Bodi hiyo, Abdul-Razaq Badru na kwamba lengo lao ni kuhakikisha wanawabaini waajiri ambao hawawasilishi kabisa madeni ya wafanyakazi hao ambao walinufaika na mkopo wa elimu ya juu na sasa wamewaajiri.
Badru amesema wanufaika wengi wa mikopo, wakiwemo wadaiwa sugu, wameonesha ushirikiano mkubwa katika kurejesha mikopo yao, hivyo kurahisisha kazi ya kukusanya madeni.
“Kiasi cha pesa za wadaiwa sugu kilichoiva na kinachotakiwa kuwasilishwa ni Tsh. bilioni 285, hii inajumuisha kuanzia kazi hii ya kukopesha ilipoanza,” amesema
“Tangu mwaka jana mpaka sasa tumewapata wadaiwa sugu 26,000, tunashukuru wanufaika hawa wamejitokeza na wanawasilisha mikopo yao. Kuna baadhi ya waajiri wanawasilisha vizuri marejesho ya wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu, wengine hawawasilishi na wengine wanawasilisha kiasi kidogo tofauti na asilimia 15 kama sheria inavyotamka,” amesema
“Kuanzia Jumatatu, Januari . 8, mwaka 2017 tutaanza kukagua taarifa kwenye payroll za waajiri wote waliosajiriwa kubaini waajiriwa wao ambao ni wanufaika wa mikopo wanaodaiwa ili waweze kukatwa,” amesema Badru.
Badru amesema wamelazimika kufungua ofisi zao nchi nzima kwa ajili kusimamia malipo ya fedha hizo za mikopo, hasa wale waliotajwa kwenye orodha ya wadaiwa sugu.
Leave a comment