SALIM Bimani, Mwenyekiti wa Kamati ya Itikadi, Uenezi, Mawasiliano na Umma wa Chama cha ACT Wazalendo, amesema kitendo cha vyama vya siasa, kuzuiwa kufanya shughuli za siasa, ni sawa na kuzuia maji kuteremka kwenye mto. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Bimani ametoa kauli hiyo leo tarehe 24 Oktoba 2019, jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na wanahabari.
“Tumeshuhudia matukio mbalimbali, ukosefu wa demokrasia, uvunjifu wa haki za binadamu na katiba unaofanywa na CCM. Ubakwaji wa demokrasia, ukiukwaji wa Katiba na Sheria ya Vyama vya Siasa,” amesema Bimani na kuongeza:
“Chama cha kisiasa kina haki ya kufanya mikutano ya hadhara, maandamano na makongamano sababu kinaeleza sera zake, mwaka wa nne huu chama cha CCM kimedhibiti vyama vingine visifanye shughuli za siasa, lakini ni bure kuzuia maji yasiteremke kwenye mto, maji yanateremka kwa kasi.”
Bimani ameeleza kuwa, hasira za vyama vya siasa kuzuiwa kufanya shughuli zake, zitaonekana katika uchaguzi ujao wa serikali za mitaa.
Amesema, vyama vya upinzani vitakipa kipigo cha mbwa koko, Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Sasa malipo ya kutuzuia, tuyaoneshe kwenye serikali za mitaa, wapate kipigo cha mbwa koko waone Watanzania hawaridhiki na hali hiyo, viongozi wote tunapaswa kushughulikia hilo,” amesema Bimani.
Leave a comment