SERIKALI ya Tanzania, kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia , imesema itatumia mkopo wa dola milioni 425 (zaidi ya Sh.985.49 bilioni), kufanya mageuzi na maboresho makubwa ya elimu ya juu ili kukuza uchumi kwa kuwa na wahitimu wanaoweza kuajirika na kujiajiri. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumatano tarehe 13 Januari 2021 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua kikao kazi cha wadau cha kujadili rasimu ya miongozo ya usalama wa mazingira na jamii katika utekelezaji wa mradi wa kuboreshaelimu ya juu na mabadiliko ya kiuchumi (HEET).
Dk. Akwilapo amesema, fedha hizo ambazo ni Mkopo kutoka Benki ya Dunia (WB) ulioidhinishwa katika mkutano wa tarehe 15 Desemba 2020, utajibu baadhi ya changamoto zilizopo katika vyuo vikuu
“Mradi unakuja kujibu baadhi ya changamoto, tunazokabiliana nazo katika vyuo vikuu nchini,” amesema Dk. Akwilapo.
Katibu Mkuu huyo amesema, miongoni mwa mambo yatakayotekelezwa katika mradi huo ni kuboresha na kujenga miondombinu mingine ya kufundishia na kujifunzia, kununua vifaa, kuhuisha mitalaa “ili kuwawezesha wahitimu kuajiliwa au kujiajili wao wenyewe.”
Amesema, mradi huo pia, utawezesha kuongeza udahili wa wanafunzi vyuoni kutoka ndani na nje ya nchi huku akikumbushia kuwa zamani Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kilikuwa kikidahili wanafunzi wengi kutoka nje.”
Dk. Akwilapo amesema, kupitia mradi huo pia, wataalamu 639 watapata mafunzo na kutakuwa na mafunzo kazini ambapo vyuo 14 za umma vitahusika katika mradi huo.
Awali, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Profesa James Mdoe alisema, lengo la kukutanisha wadau ni kupata uelewa wa pamoja ili kushauri na kuboresha kuhusu mradi huo.
Profesa Mdoe alisema, mradi wowote unahitaji kuwa na rasilimali fedha na rasimali watu na ndiyo maana walianza kutafuta fedha kuanzia Januari 2018 na kufanikiwa kuidhinishiwa mkopo huo ambao ukianza kutekelezwa, utakuwa na matunda chanya kwa nchi.
Leave a comment