WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia nchini Tanzania, Profesa Joyce Ndalichako amekagua miradi ya elimu inayotekelezwa katika Halmashauri ya Kasulu mkoani Kigoma yenye thamani ya zaidi ya Sh. 13 bilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kigoma … (endelea).
Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Kasulu, Chuo cha Ualimu Kabanga na jengo la Utawala la shule ya Sekondari Grand.
Profesa Ndalichako, amefanya ukaguzi huo jana Jumanne tarehe 30 Juni 2020.
Akizungumzia maendeleo ya ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga, Profesa Ndalichako alisema, kinajengewa upya miundombinu yote baada ya ile ya awali kuchakaa na kushindwa kukarabatiwa.
Alisema ujenzi wa miundombinu ya chuo hicho unagharimu zaidi ya Sh. 10 bilioni na utakapokamilika utabadili taswira ya mji huo kwa kuwa majengo yanayojengwa ni ya kisasa na imara ambayo yatadumu kwa muda mrefu.
Kuhusu ujenzi wa jengo jipya la utawala na utengenezaji wa mfumo wa maji katika shule ya sekondari ya Grand, Profesa Ndalichako alisema, umegharimu zaidi ya Sh. 534 milioni na kwamba utakapokamilika utaongeza morali ya walimu kufundisha na kusaidia wanafunzi waliopo katika shule hiyo.
Mradi mwingine uliotembelewa ni ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha wilaya ya Kasulu ambao upo katika hatua za mwisho ukiwa umegharimu zaidi ya Sh. 2.97 bilioni.
Alisema majengo 15 yatajengwa na kitachukua wanafunzi 320 watakaokuwa wakilala chuoni hapo.
Profesa Ndalicahko aliwataka wananchi wa wilaya ya Kasulu na mkoa wa Kigoma kwa ujumla kutumia fursa ya kuwepo kwa vyuo mbalimbali katika Halmashauri hiyo kujipatia maarifa na ujuzi utakaowawezesha kuajiriwa ama kujiajiri ili kujiletea maendeleo binafsi na ya mkoa wa Kigoma.
Awali, Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Simon Anange aliishukuru Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa namna ilivyojikita katika kupanua wigo wa elimu.
Alisema katika wilaya yake, kuna maeneo ambayo ni ya wafugaji na watoto hawakuwa wakienda shule lakini kwa sasa zimejengwa shule shikizi katika maeneo hayo ya mbali hivyo kuwezesha watoto kusoma na kuleta matokeo chanya.
Kanali Anange alisema baada ya Serikali kutekeleza Sera ya Elimu bila ada, kumekuwa na ongezeko kubwa la wanafunzi, hivyo kusababisha Serikali kupanua miundombinu katika ngazi zote za elimu ili kuwezesha fursa za masomo kwa wanafunzi ikiwemo kuongeza walimu.
Alisema ujenzi wa miundombinu mbalimbali katika sekta ya elimu itawezesha vijana wa Kitanzania kupata elimu katika mazingira bora.
Naye Mratibu wa Mradi wa Uendelezaji wa Elimu ya Ualimu (TESP), Ignas Chonya alisema ujenzi wa miundombinu katika Chuo cha Ualimu Kabanga awamu ya kwanza unatarajiwa kukamilika Oktoba 2020, chuo kitakuwa na uwezo wa kuchukua wanachuo 400 kwa wakati mmoja na kwamba chuo kinatarajiwa kuanza mafunzo mwaka huu.
Leave a comment