SERIKALI ya Tanzania imependekeza mfumo wa ukusanyaji wa mapato yanayotokana na sekta ya utalii na mazao ya misitu nchini humo kufanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa mwaka wa fedha 2020/21. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango leo Alhamisi tarehe 11 Juni 2020 Bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha bajeti ya serikali ya mwaka 2020/21 ya Sh. 34.87 Trilioni.
Dk. Mpango amesema, katika kuboresha mfumo wa ukusanyaji wa maduhuli yanayotokana na sekta ya utalii na mazao ya misitu, Serikali inapendekeza ukusanyaji wa maduhuli hayo ufanywe na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na mapato hayo yaingie katika Mfuko Mkuu wa Hazina.
Amesema, utekelezaji wa hatua hii utahusisha marekebisho katika Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania, Sura 399, Sheria ya Hifadhi ya Mamlaka ya Ngorongoro, Sura 284, Hati ya Kuanzisha Mamlaka ya Hifadhi ya Wanyamapori ya mwaka 2014, na Sheria ya Hifadhi za Taifa, Sura 282 kupitia Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2020 (The Finance Bill, 2020) ili:
(i) Kuipa TRA mamlaka kisheria ya kukusanya maduhuli yanayokusanywa hivi sasa na Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), na Mamlaka ya Hifadhi ya Wanyamapori (TAWA);
(ii) Kuweka sharti la kisheria ili kuwezesha maduhuli yatakayokusanywa na TRA yahifadhiwe Mfuko Mkuu wa Hazina badala ya utaratibu wa sasa unaoruhusu taasisi hizi kubaki na mapato yake;
(iii) Kuweka utaratibu wa kisheria kwa taasisi hizo kutumia utaratibu wa bajeti ya Serikali na kuondoa mfumo wa kibajeti unaotumiwa na taasisi hizo kwa sasa.
Leave a comment