ALBERT Chalamila, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya amewarudisha nyumbani wanafunzi wa kidato cha tano na sita wa Shule ya Sekondari Kiwanja, hadi tarehe 18 Oktoba 2019. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Pia, Chalamila ameagiza kila mwanafunzi katika shule hiyo kulipa Sh. 200,000, huku wengine wanaodaiwa kuchoma moto mabweni ya shule hiyo, kulipa Sh. 500,000 kila mmoja.
Chalamila ametoa adhabu hiyo ili kufidia gharama za ujenzi wa mabweni ya shule, yanayodaiwa kuchomwa moto na baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo.
Mkuu huyo wa mkoa ametoa adhabu hiyo leo tarehe 4 Oktoba 2019, alipotembelea shule hiyo kwa mara ya pili, baada ya jana kuwatandika viboko wanafunzi 14, wanaodaiwa kuhusika katika tukio la kuchoma moto mabweni.
“Nilipanga niwatandike kweli kweli ,mlambe mchanga na kokoto mmeze. Ili mtaje vizuri waliofanya hivyo, lakini itoshe kusema leo mtaondoka kurudi kwa baba zenu na mama zenu, na mikono ikiwawasha ili mkachome nyumba za baba na mama zenu,” amesema Chalamila na kuongeza;
“Mliochoma mabweni, nawaambia kama mna hamu na mnawashwa kuchoma vitu, mkachome nyumba za baba zenu. Kuanzia sasa nafunga form 5 na 6, mnaondoka kwenda kwenu, na ikifika saa 4 bado mnang’ang’a hapa, mtakung’utwa kichapo cha kufa mtu.”
Chalamila ameeleza kuwa, mwanafunzi atakayeshindwa kulipa fedha hizo kabla ya muda husika, atachukuliwa hatua ikiwemo kuzuiwa kufanya mtihani wa kumalizia kidato cha sita.
“Mtu yeyote ambaye hataingiza pesa kabla ya tarehe 18 na kuja kuripoti shule, utafuatwa na pingu huko huko uliko. Na jambo la pili, tutakukuzuia hautafanya mitihani tena ya kidato cha 6 katika maisha yako mpaka unaingia kaburini,” amesema Chalamila.
Leave a comment