KLABU ya Azam FC leo imemtambulisha rasmi, Arastica Cioaba kuwa kocha mkuu wa timu hiyo aliyekuja kuchukua nafasi ya Ettien Ndailagije aliyeiongoza timu hiyo muda mfupi huku akiwa Kocha wa muda wa Timu ya Taifa ya Tanzania “Taifa Stars.” Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Cioaba ambaye ni raia wa Romania ameingia mkataba wa mwaka mmoja kuifundisha timu hiyo yenye maskani yake Chamazi jijini Dar es Salaam, ikiwa ni mara ya pili ndani ya miaka miwili.
Aidha kocha huyo mwenye leseni ya juu ya ukocha ya UEFA amerejea sambamba na kocha wa viungo Costel Birsan aliyekuwa naye awali wakati anaifundisha Azam FC.
Ikumbuke hii ni mara ya pili kwa kocha huyo kujiunga na Azam FC, baada ya kufukuzwa hapo awali kutokana na timu kutofanya vizuri katika michuano ya Ligi Kuu na michuano ya kimataifa toka aliposaini mkataba Januari 5, 2017.
Azam kwa sasa itakuwa imefundishwa jumla na makocha kumi toka ilipopanda Ligi Kuu mwaka 2008 na kufanikiwa kutwaa ubingwa mara moja 2014 chini ya kocha Joseph Omog.
Leave a comment