AUGUSTINO Mrema, Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Parole, amesema kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amedhamilia kuwashughulikia wanaowabambikizia watu kesi, basi aanze na waliombambikia kesi ya kumkashifu Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa ya mwaka 1996. Anaripoti Khalifa Abdallah … (endelea).
Mrema ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour Party (TLP) amesema kama yeye alishika nafasi mbalimbali nchini ameweza kubambikiwa kesi kuwa amemtukana Rais Mkapa basi haitashindikana kwa mtanzania wa kawaida kubambikiwa kesi yoyote.
“Watu wanaposema wanabambikiwa kesi siyo uongo. Mimi niliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Naibu Waziri Mkuu nilifanyiwa hivyo, itakuwaje kwa mwananchi wa kawaida,” amesema Mrema na kuongeza:
“Jinsi Waziri Kangi Lugola alivyoanza kazi yake amenitia moyo pamoja na watanzania kwa ujumla, naweza nikasema akiendelea hivi anaweza akavaa viatu vyangu.”
Aidha, amesema Lugola ana kazi kubwa ya kufanya kwa sababu Wizara ya Mambo ya Ndani ndiyo kioo na uchafu wowote unaotaka kuuondosha katika nchi, wizara hiyo inahusika kwa kiasi kikubwa kutekeleza jukumu hilo.
Amesema yeye kama Mwenyekiti wa Bodi ya Parole bado hajajua ni asilimia ngapi ya waliokuwepo jela wamebambikiwa kesi lakini ni watu wengi.
Leave a comment