MTU mmoja anayefahamika kwa jina la Mussa Faustine (19) mkazi wa Bugarika wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza, ameuawa na wananchi wenye hasira kali kwa tuhuma za ujambazi. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 28 Julai, 2018, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, DCP Ahmed Msangi amesema Faustine amefariki dunia akiwa njiani kuelekea hospitali kutokana na majeraha ya kipigo cha wananchi, baada ya kuhojiwa na askari polisi.
Kamanda Msangi amesema kabla ya mtuhumiwa huyo umauti kumfika aliutaja mtandao sugu wa ujambazi na kiongozi wake anayefahamika kwa jina la Hamza, ambao ulipanga kutekeleza matukio mengine ya ujambazi hivi karibuni.
“Kijana huyo alitoa ushirikiano vizuri kwa askari japo alikuwa katika hali ya kujeruhiwa sana, alitoa ushirikiano na kueleza kikundi chake ambacho wanashirikiana katika kufanya na kupanga matukio ambayo walikuwa wamepanga kufanya katika siku za hivi karibuni kisha alimtaja kiongozi wake aitwaye hamza maarufu mjomba,” amesema Kamanda Msangi.
Vile vile, Kamanda Msangi amesema marehemu Faustine aliwapeleka polisi maeneo wanakoficha silaha, ambapo polisi baada ya kufanya upekuzi walikuta silaha nne zilizotengenezwa kienyeji na risasi saba.
Kamanda Msangi amesema mwili wa marehemu umehifadhiwa hospitali ya rufaa ya Bugando kwa ajili ya uchunguzi na kwamba uchunguzi ukikamilika utakabidhiwa kwa ndugu zake.
Leave a comment