ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheli (KKKT), Dayosisi ya Karagwe, Dk. Benson Bagonza, amedai muswada wa vyama vya siasa, “umeandaliwa mahususi kumlinda,” Jaji Francis Mutungi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Akichangia mjadala wa muswada wa sheria ya vyama vya siasa, jijini Dar es Salaam, Askofu Bagonza amesema, muswada huo, “haukuandaliwa kwa ajili ya wananchi.”
“Huu ni muswada ulioandaaliwa siyo kwa ajili ya wananchi; bali umeandaliwa kwa ajili ya msajili wa vyama na ofisi yake,” amesisitiza Askofu Bagonza.
Mdahalo juu ya muswada wa vyama vya siasa, uliandaliwa na chama cha mawakili – Tanganyika Law Society (TLS).
Anasema, “…kwa jinsi nilivyousoma na kusikiliza maoni ya wadau, hasa kuhusu baadhi ya vifungu vilivyomo kwenye muswada huu, nimegundua kuwa muswada mzima, haukuandaliwa kwa ajili ya vyama vya siasa wala wananchi. Umeandaliwa kwa ajili ya kumpa nguvu na mamlaka makubwa msajili wa vyama.”
Askofu Bagonza amesema, muswada huo umemtanabaisha msajili wa vyama kuwa kama malaika ambaye hakosei.
“Muswada huu umempa mamlaka makubwa msajili ambapo unamuona kama malaika ambaye hakosei wakati yeye ni binaadamu. Ndani ya muswada kumewekwa vifungu vinavyozuia msajili kushitakiwa mahakamani na hivyo kuongeza idadi ya viongozi ambao hawashitakiki,” ameeleza.
Naye Katibu wa Jumiya ya Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda, akiachangia hoja kwenye muswada huo, amesisitiza kuwapo uadilifu kwa viongozi wa umma kwa kutengeneza sheria zinazolenga kuwasaidia wananchi sio zitakazolinda madaraka yao.
Kwa upande wake, mwanazuoni mahiri nchini na mchambuzi wa masuala ya siasa, Azaveli Lwaitama, amekionya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutojiingiza katika migogoro inayoweza kuepukika.
Amesema hatua ya CCM kuruhusu serikali yake; na au kunyamazia kuwasilishwa bungeni muswada wa aina hiyo, kunakiondolea chama hicho uhalali wake mbele ya jamii.
Anasema, ni makossa kwa chama hicho kujitangaza kuwa chama tawala, kwa kuwa kutawala ni kitendo cha kuwangia watawaliwa kile anachotaka mtawala.
Anasisitiza, “ndiyo maana tunasema, Mjerumani alitawala Tanganyika. Huu muswada umesheheni vimelea vya ubaguzi. Haufai.”
Amesema, muswada umempa msajili wa vyama vya siasa mamlaka makubwa ya kuingilia hadi mambo ya ndani ya vyama vyanyewe.
Dk. Lwaitama amesema, vifungu vya muswada mpya vina sura ya kulinda maslahi ya chama fulani ambapo anaona kuwa msajili anaweza kuamua afute chama fulani kwa namna yeye atakavyoona.
Amesema, haoni sababu ya kutungwa kwa sheria itakayotoa upendeleo upande mmoja.
Leave a comment