ASKOFU wa Kanisa la Anglikana, Jimbo la Central Tanganyinya Dk. Dickson Chilongani, amewataka waumini wa Kikristo kutumia vyema kipindi cha Kwaresma kwa kuwasaidia wahitaji. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Amesema, kipindi cha Kwaresma kiwe kipindi cha toba ambacho kinaambatana na kuwasaidia watu wenye uhitaji hususani yatima, wajane na watu wanaoishi katika mazingira magumu.
Ametoa kauli hiyo tarehe 26 Februari 2020, wakati wa ibada ya kupaka majivu, muda mfupi baada ya kumalizika kwa mahubiri yaliyofanyika katika Kanisa la Anglikana linalojulikana kama Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu Jijini Dodoma.
Amesema, kipindi hiki cha kukumbika mateso ya Yesu Kristo, kiwe kipindi cha kufanya maombi ya toba kwa mtu mmoja mmoja, familia, jamii inayomzunguka pamoja na kuliombea taifa.
Naye Mchungaji Canon Jonas Mdumulla ambaye ni kiongozi wa ibada wa kiingereza akihubiri kanisani hapo, amewataka waumini wote wa Kikristo kujiepusha na maovu na badala yake wawe watu wa kuomba toba.
Pamoja na kuwataka kujiepusha na uovu na kuomba toba, pia amewakemea baadhi ya Wakristo wanaoacha dhambi katika kipindi cha Kwaresma pekee na kisha wanarudia kutenda.
“Kwa sasa kuna watu ambao wamejinyenyekeza, lakini kipindi hiki cha majivu kikiisha, wanarudia kutenda dhambi wengine wanachukua au kutoa rushwa.
“Unapokuwa kwa Kristo, unatakiwa kuwa moja kwa moja hakuna kupwa na kujaa pamoja na kuwa yapo mapito mbalimbali pamoja na majaribu lakini njia pekee ni kufanya maombi ambayo yatakuvusha katika mapito yako,” amesema.
Leave a comment