ASKOFU wa kanisa Methodist jimbo la Dodoma,Joseph Bundala amemtaka rais Dk. John Magufuli kuingilia kati suala la mfumko wa bei ya vyakula ili kuwanusuru watanzania wa kipato cha chini, anaandika Dany Tibason.
Askofu Bundala amesema kuwa kwa sasa watanzania wengi hususani wa mkoa wa Dodoma wamekuwa wanakabiliwa na mfumuko wa bei ya vyakula.
Kwa sasa watanzania wengi wanapata shida kubwa ya kununua chakula kutokana na mfumuko wa bei ya chakula wakati huo upatikanaji wa fedha ni mgumu sana.
Kuhusu mfumuko wa bei Askofu Bundala amesema taifa haliwezi kuwa na uzalishaji wa kutosha kama wananchi wenyewe wana njaa.
“Ili kupata taifa lenye watu wenye nguvu na wazalishaji wazuri ni lazima washibe na wapate chakula cha kutosha, lakini chakula kikiwa haba na watu wakakosa chakula cha kutosha ni wazi kuwa uzalishaji utakuwa mdogo.
“Kama unga wa mahindi unapanda kutoka Sh. 1,800 kwa kilo moja na kufikia Sh. 2,500 kwa kilo moja, huku kiroba cha unga wa sembe kilo 25 kilichokuwa kikiuza sh 26000 na kuuzwa sh. 40,000 huku debe la mahidi lililokuwa likiuzwa sh.18,000 na sasa kuuzwa Sh. 30,000 hapo unawezeje kusema hakuna njaa.
“Wakati mwingine siyo dhambi kusema kuwa taifa lina njaa kwani mambo mengine yapo nje ya uwezo wa mwanadamu ni kutokana na mabadiliko ya tabia ya nchi hivyo yanapotokea majanga kama hayo nilazima serikali ikajipanga kuwakomboa wananchi wake,” amesema Askofu Bundala.
Akizungumzia suala la njaa askofu Bundala,alisema kuwa siyo kweli kwamba nchi haina njaa bali viongozi wamejazwa hofu ya kutokusema ukweli juu ya suala hilo jambo ambalo ni hatari kwa mstakabali wa taifa.
Hata hivyo kiongozi huyo aliwaasa wananchi wale ambao bado wanacho chakula cha kutosha kuhakikisha wanakitunza ili kujiwekea hakiba.
“Wale wenye akiba ya chakula hakikisha mnakitunza vizuri ili kujiwekea hakiba ya chakula, msitumie chakula kwa kupikia pombe au kufanya sherehe ambazo hazina tija kwa kutumia chakula,” amesema Askofu Bundala.
Baadhi ya wananchi ambao walizungumza walithibitisha kuwa kuna shida kubwa ya upatkanaji wa chakula huku wakieleza kusikitishwa na pandaji wa bei ya vyakula.
Leave a comment