MIONGONI mwa majimbo magumu katika uteuzi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ni Jimbo la Arusha Mjini. Anaandika Mwandishi Wetu…(endelea).
‘Vyuma vinne’ vimekutana kwenye jimbo hilo. Kitu kinachonogesha ni kwamba, wapo waliotoka upinzani na kukimbilia CCM, nao wamejitosha na kukutana na ‘wenyeji’ wa chama hicho.
Kalist Lazaro, aliyekuwa Meya wa Jiji la Arusha kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ni miongoni mwa watia nia wa ubunge katika jimbo hilo kupitia CCM.
Lazaro alikuwa na cheo cha Meya wa Jiji hilo, alihiyari kupoteza nafasi hiyo kubwa na kujiunga na CCM, leo anataka ndoto yake itimie.
Lazaro kwenye tanuri la kura ya maoni anakutaa na kijana Mrisho Gambo, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha. Gambo alitimuliwa ukuu wa mkoa huo na Rais John Magufuli hivi karibuni.
Gambo anayetaka ubunge wa jimbo hilo, anakutana na Lazaro aliyeacha umeya akiwa a mipango yake ya baadaye ikiwemo ubunge.
Kila mmoja anataka kupona maumivu yake – Gambo kutemwa ukuu wa mkoa, Lazaro kuutema umeya.
Wawili hao wanajikuta kwenye tanuri hilo na Samson Mwigamba.
Soma zaidi hapa
Oktoba 2017, Mwigamba aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo alitimikia CCM.
Hata hivyo, ni kama aliyesahaulika vile, sasa anajaribu ndoto yake ndani ya chama hicho.
Kabla ya kuingia ACT-Wazalendo, Mwigamba aliwahi kuwa Katibu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Mkoa wa Arusha na ndiye aliyeshirikiana na Zitto Kabwe, Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo kuanzisha chama hicho.
Ukitaja viongozi watano waanzilishi wa ACT-Wazalendo, majina ya Prof. Kitila Mkumbo (Katibu Mkuu Wizara ya Maji), Anna Mgwhira (Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro), Zitto na Migamba huwezi kuyaweka pembeni huku Wakili Albert Msando akiwa mwanasheria wa chama hicho.
Wakili Msando anaongeza ugumu wa kupatikana kwa mgombea wa jimbo hilo. Tayari amechukua fomu kama walivyofanya Mwigamba, Gambo, Lazaro na makada wengine.
Jimbo hilo, mpaka mchana wa leo tarehe 15 Julai 2020, jumla ya wanachama 53 wa CCM wamechukua fomu na kurejesha, ni baada ya kukidhi matakwa ya ujazaji fomu hizo.
Baada ya mchujo, mmoja kati ya hao 53 atakwenda kuvaana na Godbless Lema, mbunge wa jimbo hilo ambaye anamaliza muda wake.
Soma zaidi hapa
Tayari Lema kwenye ukurasa wake wa twitter amesema, angetamani ashindane na watia nia wote wa CCM kwenye jimbo hilo na kwamba, atashinda.
“Nimesikia sikia majina ya wagombea Ubunge Arusha Mjini kupitia CCM. Kama sheria ingeruhusu, wote 30 kushindana nami na picha zao wote kutokea kwenye karatasi ya kura dhidi yangu, bado wangeimba wimbo walioimba 2010/2015. Twendeni mpaka mwanzo wa bahari, wepesi sana hawa,” ameandika Lema kwenye ukurasa wake wa twitter jana tarehe 14 Julai 2020.
Pia Lema ni Mwenyekiti wa Kanda ya Kaskazini inayojumuisha mikoa ya Arusha, Manyara, Kilimanjaro na Tanga.
Leave a comment