DANIEL Maleki (30), aliyechana kitabu kitukufu cha Qur’an, wilayani Kilosa katika Mkoa wa Morogoro, amefukuzwa kazi rasmi leo tarehe 11 Februari 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tamko la kutimuliwa kazi Maleki, aliyekuwa mtumishi wa serikali katika Halmashauri ya Kilosa, limetolewa na Rais John Magufuli wakati wa uzinduzi wa wilaya mpya ya Kigamboni.
Awali, Suleima Jaffo, Waziri Ofisi ya Rais Twala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), alitoa tamko la kusimamishwa kazi kwa kijana huyo. Tukio la Maleki kuchanga Qur’an lilitokea tarehe 6 Februari 2020.
Siku nne baada ya tukio hilo, Sheikh Ponda Issa Ponda, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, alitoa waraka uliobeba hoja nne kutokana na tukio hilo.
Miongoni mwa hoja hizo, hoja namba tatu ilieleza “Waziri wa Tamisemi abadilishe tamko lake la kumsimamisha kazi Daniel Maleki, badala yake atamke kufukuzwa kazi.”
Sheikh Nurdeen Kishki, muandaaji wa mashindano makubwa ya Qur’an nchini, alisema kitendo alichofanya Malenki kinahitaji kulaaniwa na kila Mtanzania.
“Hakuna dini inayoruhusu kashfa ya namna hiyo, kejeli ya aina hiyo na dharau ya aina hiyo. Tumeona Daniel ametiwa mbaroni na amepelekwa mahakamani…, serikali naiomba isifumbe macho hata kidogo kwa watu kama hawa wanaotuletea chokochoko,” amesema Sheikh Kishki.
Akizungumza kwenye uzinduzi wa wilaya hiyo, Rais Magufuli amemuagiza Waziri Jaffo, kumwandikia barua rasmi ya kumfukuza kazi.
Rais Magufuli amesema, hata kama mtumishi huyo atashinda kesi kuhusu sakata hilo, uamuzi wake ni ule ule wa kufukuzwa kazi.
“Nilimsikia Jaffo anasema, mtu mmoja kule Kilosa alichana kitabu kitakatifu, nakushukuru ulichukua hatua ya kumsimamisha lakini mimi namfukuza kazi moja kwa moja.
“Umwandikie barua ya kufukuzwa kazi moja kwa moja, ashinde kesi asishinde. Umechukua jukumu la kumsimamisha kazi, mimi namfukuza,” amesisitiza Rais Magufuli.
Tukio la Maleki kuchanga Qur’an huku akitoa mameno ya kashfa, kiliteka mitandao ya kijamii na kuonsha kukera wengi kutokana na utamaduni uliojengeka nchini wa kuheshimiana katika imani za kidini.
Leave a comment