IDARA ya Uhamiaji nchini, imemkamata Jasmin Ngongolo, mkazi wa Dar es Salaam akiwa na stika za Viza 2,546 za Tanzania za kughushi. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Mwanamke huyo alikamatwa tarehe 02 Agosti 2019 saa saba usiku katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere, jijini Dar es Salaam (JNI) akitokea Afrika Kusini.
Samwel Mahirane, Kamishna wa Uhamiaji Usimamizi na Udhibiti wa Mipaka amesema, mtuhumiwa huyo alifunga mizigo hiyo kwa ustadi ikiwa na utambulisho juu ya kila boksi kuwa ni stika zinazobandikwa katika vioo vya magari.
Amesema, mtuhumiwa alikutwa na bidhaa nyingine ambazo ni sabuni za kuogea, sabuni za unga za kufulia, pampers, herein, pafyumu na vipodozi vya aina mbalimbali kwa lengo la kuwahadaa maofisa wakati wa upekuzi.
“Tumefanikiwa kumkamata pia na mume wa mtuhumiwa ambaye ni Zakayo Stanslaus na anahusishwa na hujuma hiyo kwa kufika uwanja wa ndege kwa ajili ya kumpokea mtuhumiwa,” amesema.
Inaelezwa, kukamatwa kwa watuhumiwa hao kunafuatia taarifa kutoka kwa wasamaria wema na kwamba, baada ya kukamilika kwa uchunguzi, watuhumiwa hao na watakaohusishwa na mtandao huo, watafikishwa mahakamani.
Leave a comment