FESTO Msalia mfanyabiashara wa vinywaji mkoani Dodoma amejiua kwa kujipiga riasasi kichwani kwa madai kuwa ameumizwa na kitendo cha Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma kukamta shehena yake ya pombe za viroba alizokuwa akiziuza,anaandika Charles William.
Serikali ya Tanzania imepiga marufuku uuzwaji wa pombe kali aina ya viroba kwa madai kuwa inasababisha uharibifu wa mazingira kutokana na kufungwa katika mifuko ya plastiki. Marufuku hiyo imesababisha hasara ya mabilioni ya fedha kwa wafanyabiashara wengi.
Tarehe 03 Machi mwaka huu ikiwa ni siku mbili baada ya serikali kuanza operesheni ya kukamata pombe aina ya viroba, Festo anayefanya biashara zake eneo la Dodoma Mjini alikamatwa akiwa na shehena ya tani 1.5 ya pombe hizo, ambzo sasa zinashikiliwa na polisi.
“Alijiua kwa risasi eneo la Veyula, nje kidogo ya mji wa Dodoma. Polisi walipata taarifa na walipoenda eneo la tukio waliokota maganda matano ya risasi na kumuwahisha hospitali mfanyabiashara huyo hata hivyo alikuwa tayari amefariki,” ameeleza Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma.
Serikali imekuwa ikilaumiwa kwa kutoa amri ya ghafla ya kupiga marufuku uuzwaji wa pombe za viroba bila kuzingatia kiasi cha ukubwa wa mzigo ambao wafanyabiashara hiyo walikuwa nao. Imekuwa ikielezwa kuwa kitendo hicho kinaweza kuwakatisha tama wawekezaji hapa nchini.
Serikali pia imekata kutoa ruhusa kwa wafanyabiashara hao kuzifunga upya pombe hizo katika chupa ikiwa sababu kuu ya marufu yao ni uchafuzi wa mazingira kupitia mifuko ya plastiki. Imekuwa ikilitumia jeshi la polisi kukagua madukani na kukamata pombe hizo pamoja na wafanyabiashara.
Leave a comment