WATU watano waliofariki kwenye ajali ya gari iliyotokea jana usiku tarehe 31 Agosti 2019, Kibiti mkoani Pwani sasa kufanyiwa uchunguzi wa vinasaba (DNA). Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Ajali hiyo ilihusiha Lori la Kampuni ya Dangote, lililokuwa likitoka Dar es Salaam kwenda Mtwara kugongana na gari ndogo aina ya Toyota Premio, lililokuwa likitoka kwenye nyumba za walimu wa Shule ya Sekondari ya Kibiti eneo la Kinyanya.
Taarifa zinaeleza kuwa Lori hilo likiwa limebeba malighafi za kutengeneza saruji ambapo watu watano walifariki ikiwa ni watu wazima wanne na mtoto mmoja ambayo waliteketea kwa moto.
Baada ya gari hizo kugongana, Lori lilipoteza mwelekeo na kwenda kugonga nguzo ya umeme hivyo kusababisha kuwaka moto na kuwateketeza watu hao watano.
Akizungumza na waandishi wa habarai leo tarehe 1 Septemba 2019, Aminiel Aligaesha, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) amesema, hospitali hiyo tayari imefanya uchunguzi na kuchukua sampuli kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kitengo cha Forensic Pathology pamoja na Mkemia Mkuu wa Serikali ili kufanya uchunguzi zaidi.
“Tunawaomba ndugu wa karibu wa marehemu hawa hususani Baba, Mama na Watoto kujitokeza kuanzia kesho tarehe 2 Septemba 2019 saa mbili asubuhi, kuchukuliwa sampuli na Mkemia Mkuu wa Serikali ili kusaidia kufanya uchunguzi wa kulinganisha vinasaba,” amesema.
Pia Aligaesha amesema, majeruhi wa ajali ya moto iliyotokea mkoani Morogoro ambao walikua wanapatiwa matibabu hospitalini hapo, wamebaki 11 baada ya Asha Ally Seleman (28) kupoteza maisha tarehe 28 Agosti 2019 na Avelina Pastory Aman (30) aliyefariki tarehe 31 Agosti 2019.
“Kati ya majeruhi 11 wanaoendelea kutibiwa MNH, sita wapo wodi namba 22 ya Sewahaji, watano ICU na mwili mmoja wa Avelina pastory Aman (30) ambao upo chumba cha kuhidhia maiti ukisubiri taratibu za kusafirishwa kwenda Morogoro kwa ajili ya mazishi. Kati ya majeruhi 47 walifikishwa hospitalini hapa 36 tayari wamefariki,”amesema.
Leave a comment