WATU zaidi ya watano wamepoteza maisha huku 26 wakijeruhiwa katika ajali ya basi iliyotokea leo Ijumaa tarehe 21 Agosti 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kagera … (endelea).
Ajali hiyo imetokea kwenye mteremko wa Kyamalebe wilayani Muleba Mkoa wa Kagera.
Taarifa ya ajali hiyo imetolewa na Revocatus Malimi, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Kagera, wakati anazungumza na wanahabari.
Kamanda Malimi amesema, chanzo cha ajali hiyo ni basi la Kampuni ya Sabuni lenye namba ya usajili T 392 AZB lililokuwa likielekea jijini Mwanza kupinduka wakati likitokea eneo la Nshamba wilayani Muleba.
Amesema majeruhi wanne kati ya 26 hali zao ni mbaya huku waliosalia wakiendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali Teule ya Rubya na Hospitali ya Ndolage.
“Kwa mujibu wa mashuhuda walioshuhudia maiti ambazo tuna taarifa zao ni watano,” amesema Kamanda huyo na kuongeza huko walikopelekwa kwa matibabu yawezekana vifo vikaongezeka
Kamanda huyo wa Polisi amesema, uchunguzi wa awali unaonesha dereva alikuwa mwendo kasi kitendo kilichosababisha gari kumshinda katika kona ya mteremko huo.
“Uchunguzi wetu wa awali na jiografria ya eneo hili ingawa chanzo cha ajali hakijafahamika, lakini zipo dalili za wazi kwamba kwa vyovyote vile, gari litakuwa mwendo kasi na kona iliyokuwepo hapa, lilimshinda dereva likapinduka,” amesema Kamanda Malimi.
Amesema Jeshi la Polisi lina endelea kumtafuta dereva wa gari hilo, ambaye baada ya kutokea alikimbilia kusikojulikana.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online, MwanaHALISI TV na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali
Leave a comment