KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Bashiru Ally, ameahidi kuwapitisha kwenye ‘tanuri’ wagombea wa chama hicho kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa utaofanyika tarehe 24 Novemba 2019. Anaandika Regina Mkonde…(endelea).
Akihojiwa na gazeti moja la kila siku, Dk. Bashiru amesema, mwanachama yeyote wa chama hicho anayetaka kugombea nafasi ya uenyekiti wa mtaa au wa kijiji, atajadiliwa na kamati ya siasa ya tawi.
Na kwamba katika mchakato wa kuteua wagombea, hakutakuwa na mianya ya rushwa wala upendeleo, bali utafanyika kwa uwazi kwa kuzingatia misingi ya demokrasia.
“Kabla ya kupigiwa kura za maoni, atajadiliwa kwanza na kamati ya siasa ya tawi lake na kamati ya siasa ya kata na hatimaye kamati ya siasa ya wilaya itafikiria na kuteua majina ya WanaCCM wasiozidi watatu kwa kila kijiji.
“… ama mtaa walioomba kugombea uenyekiti wa kijiji ama mtaa ili wakapigiwe kura za maoni na mkutano wa wanachama wote katika tawi husika,” amesema Dk. Bashiru.
Dk. Bashiru amesema baada ya wahusika kujadiliwa na kamati ya siasa ya tawi au kata, wanachama wa eneo husika watawapigia kura za maoni kwa ajili ya kumpata MwanaCCM atakayepeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi huo.
Leave a comment