CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimetuma mawakili wake kwenda kufuatilia ukweli kuhusu taarifa za ugonjwa wa Freeman Mbowe, mwenyekiti wa chama hicho Taifa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Salum Mwalimu, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Visiwani akizungumza na mwandishi wa habari hizi leo asubuhi tarehe 18 Januari 2019 amesema, hawakuwa na taarifa hivyo chama hicho haraka kimeona umuhimu wa kuunda timu ya mawakili wake ili kufuatilia afya yake.
“Hatukujua awali, habari za kuumwa kwake tumezipata jana mahakamani. Kutokana na taarifa hiyo, tumeona kuna kila sababu ya kwenda kujua ukweli wa taarifa hiyo. Taarifa ya ugonjwa wake imeletwa na mawakili wa serikali na sio sisi,” amesema.
Taarifa ya ugonjwa wa Mbowe ambaye ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni pia Mbunge wa Hai ilipelekwa na Wakili Mkuu wa Serikali, Patrick Mwita jana mahakamani hapo.
Mbowe na viongozi wengine wa chama hicho wanakabiliwa na tuhuma za kufanya maandamano na mikusanyiko kinyume na sheria.
Mwalimu amesema kuwa, baada ya mawakili hao kwenda gerezani na kumjulia hali ndio watapata ukweli wa nini kinamsumbua na kisha watajua nini cha kufanya.
“Nini tutafanya itatokana na taarifa ya mawakili ambao wataenda kumjulia hali,” amesema Mwalimu.
Mbowe na Ester Matiko wamendelea kuwekwa rumande baada ya dhamana yako kukataliwa tarehe 23 Novemba 2018 kwa madai ya kukiuka masharti.
Leave a comment