PIKIPIKI na Bajaji zinazosafirisha abiria, zimeruhusiwa kuingia katikati ya Jiji la Dar es Salaam, ili kupunguza changamoto ya usafiri katika kipindi cha mlipuko wa Ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Zuio la Pikipiki kwa jina maarufu Bodaboda na bajaji kuingia mjini, limeondolewa leo tarehe 1 Aprili 2020, na Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, wakati akizungumza na wanahabari.
“Kwa sababu ya uhaba wa usafiri,nimeruhusu bodaboda zote na bajaji kuingia katikati ya jiji,kwa kipindi hiki ambacho tunapambana na Corona,” amesema Makonda.
Aidha, Makonda amesema atamuandikia barua Seleman Jaffo, Waziri wa Ofisi ya Rais- TAMISEMI, kumuomba ruhusa ya mabasi 200 ya mwendokasi yaliyokwama katika bandari kavu kutokana na mgogoro, kuingia barabarani.
Kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19, serikali imepiga marufuku daladala kubeba abiria wengi kuliko idadi ya viti vya daladala hizo, ili kuepusha misongamano inayoweza sababisha watu kuambukizana ugonjwa huo.
Marufuku hiyo imesababisha changamoto ya usafiri kutokana na uhaba wa mabasi ya abiria, hasa abasi ya mwendokasi
Hadi sasa, serikali kupitia wizara ya afya, imeripoti wagonjwa 19 walioambukizwa ugonjwa huo, ambapo mtu mmoja kati yao amefariki dunia jana tarehe 31 Aprili 2020, akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Mloganzila, jijini Dar es Salaam.
Leave a comment