Saturday , 20 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa ACT- Wazalendo yagawanyika
Habari za Siasa

ACT- Wazalendo yagawanyika

Spread the love

UAMUZI wa Kamati Kuu (CC) ya chama cha ACT- Wazalendo, kujiunga kwenye serikali ya Umoja wa Kitaifa Visiwani (SUKI), umeanza kupingwa kila kona. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Baadhi ya waliojitokeza kupinga ushirika huo, ni pamoja na aliyekuwa rais wa chama cha wanasheria Tanganyika (TLS), Fatma Karume; aliyekuwa mgombea ubunge wa chama hicho, katika jimbo la Nyamaga, jijini Mwanza, Adams Chagulani na mwanaharakati wa mitandaoni, Maria Sarungi.

Wengine, ni baadhi ya wanachama wa chama wa kawaida, wafuasi na wanaharakati kadhaa kutoka Zanzibar na Bara.

Akiandika katika ukurasa wake wa twitter, Fatma ambaye anafahamika sana kwa jina la Shangazi anasema, “…mwanzo wa mwisho wa ACT- Wazalendo. Someni historia ya Zimbabwe na Tsvangirai.”

Anasema, “Maalim (Seif Shariff Hamad) anaaga. Hii ndio miaka yake mitano ya mwisho.” Anahoji, “nani ataweza kuhamasisha umma mwaka 2025?”

Maalim Seif Sharrif Hamad, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo

Fatma, mmoja wa watoto wa aliyekuwa rais wa Zanzibar, Aman Abeid Karume amesema, “bora mngeanza ku-Comprise kabisa na Hussen leo ili Mkurugenzi atakugaienni firigisi au shingo mwaka 2015, paja na kifua ndio basi.

Naye Chagulani ameeleza kuwa anapinga maamuzi hayo kwa kuwa hayana faida kwa chama na watu wake, hasa Tanzania Bara.

“Sikubaliani na kilichoamuliwa na chama changu cha ACT- Wazalendo. Uharamu wa vyama ya nguruwe hauondoki kwa kuweka vitunguu swaumu over,” ameandika Chagulani katika ukurasa wake wa twitter.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, leo Jumapili, katibu mkuu wa chama hicho, Ado Shaibu alisema, chama chake kimeamua kuingia kwenye serikali, kushiriki baraza la wawakilishi na kuingia bungeni.

Zitto Kabwe, Kiongozi wa ACT-Wazalendo

Alisema, “katika mkutano maalum wa kamati kuu, tumeamua kupendekeza jina la mwanachama atakayekuwa makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar. Tumeruhusu wajumbe wa baraza la wawakilishi, wabunge na madiwani waliochaguliwa kukiwakilisha chama na wananchi waliowachagua.”

Amesema, miongoni mwa sababu walizotoa kufikia uamuzi huo, ni pamoja na kutathimini historia ya mapambano ya demokrasia Visiwani  na Bara.

Aidha, Ado amesema, chama chake kimefikia maamuzi hayo, kwa kurejea matukio kaadha ya raia kujeruhiwa, uwepo wa uhasama wa kisiasa, kudhalilishwa kijinsia na mali za watu kuharibiwa.

Amesema, Kamati Kuu imeeleza kuwa katika uchaguzi mkuu uliyoisha, watu 17 walifariki dunia.

Katika baadhi ya mitandao ya kijamii, wengi wa wanaopinga maamuzi hayo wanaekekeza hoja yao kwenye msingi wa kurejesha nyuma harakati za mapambano, ikiwamo madai ya tume huru ya uchaguzi, katiba mpya na uwapo wa utawala sheria.

Akichangia hilo, mmoja wa wanachama wa ACT- Wazalendo amesema: “Asili ya siasa ni mapambano. Sasa kama mapambano yako yamelenga kuangalia maslahi binafsi, na siyo maslahi ya walioathirika, basi ni shida.”

Mwingine anasema, “wengi wa Wazanzibari, wanahitaji chama mbadala. Wanaamini kuwa CCM, si chama kinachowahitaji. Lakini maamuzi ya Kamati Kuu leo, hayaleti picha ya kutafuta mbadala. Yanaonyesha kuna malengo ya kupoza njaa.”

Mchangiaji ambaye amejitambulisha kuwa  mwanachama wa chama hicho anasema, “kama wakati wa kupigania uhuru, lengo lilikuwa kujiunga na wakoloni, uhuru usingepatikana. Lakini tulifanikiwa kupata uhuru kwa kuwa lengo letu lilikuwa kumuondoa mkoloni, bila kujali itachukua muda gani.”

Kupatikana kwa taarifa kuwa ACT- Wazalendo, imeridhia kuingia serikali, kushiriki Bunge na Baraza la wawakilishi, kumekuja miezi kadhaa, tokea Kiongozi Mkuu wa chama hicho, Zitto Zuberi Kabwe, kutangaza kuwa chama chake, hakitambui uchaguzi mkuu uliyopita na hivyo, hakitashiriki kwenye serikali.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Dk. Mwakyembe : Zanzibar waliongoza kutaka Serikali 2 za muungano

Spread the love  MWANASIASA mkongwe nchini, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema mjadala wa...

Habari za SiasaTangulizi

Rais Samia ataja mikakati ya kufikia trilioni 2 biashara Uturuki, Tz

Spread the loveWakati Tanzania na Uturuki zikidhamiria kuongeza kiwango cha biashara hadi...

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

error: Content is protected !!