CHAMA cha ACT-Wazalendo kimetilia shaka maelezo ya Jeshi la Polisi kuhusu mauaji ya kijana Isaka Petro aliyofanyika katika Kanisa la Sabato wilayani Itigi, Singida. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 8 Februari 2019 Ado Shaibu, Katibu wa Itikadi, Mawasiliano na Uenezi wa chama hicho amesema, maelezo ya polisi yametofautiana na yale ya mashuhuda wa tukio hilo.
Akinukuu maelezo ya polisi amesema, wameueleza umma kuwa Pius Luhende, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Itigi hakuwa ndani ya kanisa wakati mauaji hayo yanafanyika hivyo yeye siye mtu aliyemfyetulia risasi Petro.
“Maelezo ya Jeshi la Polisi yamekwenda kinyume na maelezo ya ndugu wa marehemu na waumini wote waliokuwepo ndani ya kanisa siku ya Jumamosi ya Tarehe 2 Februari mwaka huu wakati mauaji hayo yakifanyika” ameeleza Ado.
Amesema kuwa, baba wa marehemu na waumini wa kanisa hilo wanasema kuwa, wamemshuhudia mkurugenzi Luhende akimfyatulia risasi Petro.
Amesema kuwa, Jeshi la Polisi halitawatendea wananchi haki kwa kufanya hivyo “ni jambo linalofedhehesha kwamba, Jeshi la Polisi linajaribu kufanya hila ili kupindisha haki kwenye tukio hilo la mauaji ya kinyama yaliyofanyika kwenye nyumba ya mungu.”
Amesisitiza kuwa, chama hicho chenye sera za uwazi kinataka kuona haki ikitendeka bila kujali cheo cha mtu yoyote “hakuna aliyekuwa juu ya sharia.”
unaweza kutizama video hapo chini
Leave a comment