SERIKALI imekwama kushawishi wananchi kujitokeza kujiandikisha katika daftari la wapiga kura, jambo ambalo linaleta taswira hasi kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa baadaye mwaka huu. Anaripoti Martin Kamote…(endelea).
Joran Bashange, Mwenyekiti wa Kampeni na Uchaguzi Taifa wa Chama cha ACT-Wazalendo ametoa kauli hiyo leo tarehe 15 Oktoba 2019, alipozungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi ndogo za chama hicho jijini Dar es Salaam.
Amesema, chama hicho kimekuwa kikifuatilia kwa makini mchakato wa uandikishaji tangu mwanzo, na kwamba mwitikio hafifu wa wananchi unatoa ujumbe mkubwa kwa Serikali ya Rais John Magufuli.
“Tumekuwa tukifuatilia mchakato wa uandikishaji wa wananchi katika maeneo mbalimbali ya nchi, kumewa na mwitikio mdogo sana,” amesema.
Amesema, chama hicho kilifanya juhudi kuhamasisha wananchi kujiandikisha, hata hivyo juhudi hizo zilikumbana na vikwazo kutoka Jeshi la Polisi.
“Chama chetu kiliendelea na njia mbadala zikiwemo kusambaza vipeperushi na kutumia Radio za kijamii katika maeneo mbalimbali za nchi, ili kufikisha ujumbe kwa wananchi wajiandikishe,” amesema.
Kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo ametoa wito kwa Jeshi la Polisi kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa sheria za nchi, ikiwa ni pamoja na kujiepusha ushabikiwa kisiasa.
“Tunamtaka IGP (IGP Simon Sirro) aliongoze jeshi la polisi liwe la kwanza kutii sheria bila shuruti, badala ya kuimba ngonjera kwa umma,” amesema.
Leave a comment