ANNA Mghwira, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo amekabidhiwa Ilani ya CCM baada ya kuapishwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Ikulu leo, anaandika Hamisi Mguta.
Mghwira amekabidhiwa Ilani hiyo na Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Tanzania Bara) Rodrick Mpogolo ikiwa ni sehemu ya Katiba ya CCM, kuwa Mkuu wa Mkoa ni sehemu ya chama hicho na anashiriki kikao cha kamati ya siasa ya mkoa.
Kutokana na tukio hilo Uongozi wa chama cha ACT-Wazalendo kesho inatarajia kukutana kutafakari namna Anna Mghwira, Mwenyekiti wa chama hicho atakavyotekeleza majukumu ya nafasi hiyo na Ukuu wa mkoa.
Ado Shaibu, Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa chama hicho amesema uamuzi huo ni baada ya Mghwira kufanya mazungumzo na viongozi wenzake wa juu wa chama kuhusu uteuzi wake.
“Kufuatia uteuzi huu na kwa kuzingatia unyeti na majukumu ya mkuu wa mkoa, Kamati ya Uongozi wa chama itakutana Juni 7, 2017 kutafakari pamoja na mambo mengine, namna ambavyo mama Anna Mghwira atatekeleza wajibu wake wa uenyekiti wa chama na majukumu yake mapya,” amesema.
https://www.youtube.com/watch?v=qPRUYeWzcXY
Mgwira ambaye alikuwa mmoja wa wapinzani wa Rais Magufuli katika uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 anachukua nafasi aliteuliwa na rais kushika wadhifa huo Juni 3, mwaka huu.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanaeleza kuwa uteuzi huo ni anguko kwa ACT-Wazalendo kwani Mkuu wa Mkoa anatambulika kama Mjumbe wa Kamati ya siasa (CCM) hivyo Mghwira atalazimika kukiacha chama hicho na kutimkia CCM.
Ikumbukwe kuwa uteuzi huo ndani ya chama hicho ni wa pili unafanyika na Rais Magufuli kuingiza wapinzani katika serikali baada ya Prof. Kitila Mkumbo aliyeteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji.
Leave a comment