ZIMEBAKI siku mbili kwa Abdul Nondo, Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) kurejea chuoni (Chuo Kikuu cha Dar es Salaam-UDSM) baada ya hekaheka na hata kusimamishwa chuo. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Nondo anatarajiwa kuripoti chuoni hapo tarehe 4 Januari mwaka huu, “taratibu zote zimekamilika na sasa najiandaa kurejea chuoni kesho kutwa (Ijumaa) kwa kuwa, hakuna kizuizi chochote,” amesema Nondo leo tarehe 2 Januari 2019.
Nondo alikumbana na hekaheka na hatimaye kufikishwa mahakamani kwa madai ya kujiteka na baadaye alikutwa Iringa ‘ametupwa’ jambo ambalo lilidaiwa ni la kutengeneza.
Nondo awali alishtakiwa mahakamani Iringa akidaiwa kufanya kosa la kusambaza taarifa za uongo kupita mtandao wa WhatsApp na kumdanganya Ofisa wa Polisi kwenye Kituo cha Polisi cha Mafinga kwamba, alitekwa.
Nondo alidaiwa kutenda kosa hilo tarehe 7 Machi mwaka jana akiwa eneo la Ubungo Jiji Dar es Salaam na Mafinga mkoani Iringa.
Baada ya vuta nikuvute za kisheria kwa muda mrefu mahakamani, tarehe 5 Novemba mwaka jana Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa ilimwacha huru Nondo kutokana na upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha mashtaka yake mahakamani hapo.
Akieleza taratibu za kurejea chuo Nondo ameuambia mtandao huu kwamba, anatarajiwa kurejea chuoni hapo ili kumalizia muhula wake wa tatu.
Amesema miongoni mwa taratibu alizofanya na kurejeshwa chuoni hapo ni pamoja na wakili wake Jebra Kambole kuandika barua kwa mkuu wa chuo pamoja na kuambapatinsha vielelezo vyote. Hata hivyo uongozi wa UDSM umethibitisha kurejea kwake.
Leave a comment