HATUA ya Jecha Salum Jecha, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), kuchukua fomu ya kugombea urais kupitia CCM imeibua maswali. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaa…(endelea).
Abdul Nondo, Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana wa ACT-Wazalendo leo tarehe 21 Juni 2020 akizungumzia hatua ya Jecha kuchukua fomu ya kuwania kuteuliwa na chama chake kugombea urais visiwani humo ni sawa na refa kuishiwa uvumilivu na sasa anataka kwenda kufunga goli mwenyewe.
Amesema, Jecha ambaye alikuwa Mwenyekiti wa ZEC na aliyetangaza matokeo ya uchaguzi Zanzibar 2015, hakupaswa kujihusisha na siasa.
Mwanasiasa huyo kijana amesema, tafsiri ya wazi anayoiacha Jecha ni kwamba, katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 na sasa hakuna Tume Huru ya Uchaguzi.
Jana tarehe 20 Juni 2020, Jecha amechuku fomu ya kugombea urais na kuwa kada wa 14 kujitokeza kuomba ridhaa ya chama hicho kumpitisha visiwani Zanzibar.
Akizungumzia kitendo hicho, Nondo ameeeleza kuwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 74,14 inakataza wasimamizi wa uchaguzi katika ngazi zote kujihusisha na siasa.
“Tume zetu si Huru kwasababu wanaoteuliwa kusimamia uchaguzi, ni wazi ni makada wa Chama Cha Mapinduzi na wanapewa maagizo wafanye vile ambavyo wanavyoelekezwa.
“Hili tumeiona hata kwa aliyekuwa marehemu Jaji Augustine Ramadhani ambaye 2005 alikuwa Makamu Mwenyekiti wa ZEC na baadaye 2010 akawa Makamu Mwenyekiti wa NEC, lakini 2015 alichukua fomu kupitia CCM ya kugombea nafasi ya urais Zanzibar,” amesema Nondo.
Amesema, kitendo cha Jecha kuchukua fomu hiyo, kinadhihirisha kuwa Maalim Seif Sharif Hamad, aliyegombea urais visiwani humo kupitia Chama cha Wananchi (CUF), malalalamiko yake ya ushindi na kupokwa na ZEC yana mashiko.
“Kuna mtu anaitwa Mohammed Hija Mohamed, alikuwa Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa ambayo inatakiwa iwe inajitegemea, lakini amechukua fomu ya kutia nia kugombea urais Zanzibar kwa tiketi ya CCM.
“CCM imetutukana kwa kudhihirisha rangi ya tume zetu za uchaguzi ambazo tunazo (NEC na ZEC), kwamba ni makada watiifu wa chama,” amesema.
Hata hivyo Nondo alipoulizwa pengine Jecha aliamua kujiunga na CCM baada ya kutoka kwenye madaraka ya uenyekiti wa ZEC, amesema kuwa hakuna sehemu yoyote ambayo imetangazwa wala kusikika kuwa amejiunga na CCM wala kuchukua kadi ya uanachama hivyo inaonyesha alikuwa mwanachama wa muda mrefu.
Leave a comment