MBUNGE wa Kyadondo Mashariki nchini Uganda, Robert Kyagulanyi maarufu kama ‘Bobi Wine’ amekamatwa na Jeshi la Polisi alipowasilisi katika Uwanja wa Ndege wa Entebbe akitokea nchini Marekani alikokuwa anapatiwa matibabu. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Polisi nchini humo wamenukuliwa na vyombo vya habari wakisema kuwa, Bobi Wine hajapewa kibali cha kufanya mkutano au shughuli yoyote, ambapo Msemaji wa polisi mjini Kamapala, Luke Owoyesigyire, alionya kuwa yeyote atakayeshiriki kwenye shughuli yoyote inayomhusu Bobi Wine atakamatwa.
Hadi sasa inadaiwa ndugu wa Bobi Wine anayefahamika kwa jina la Eddy Yawe na Naibu Msemaji wa chama cha Democratic Party, Waiswa Alex Mufumbiro, walikamatwa na vikosi vya usalama na kuzuiwa kwenye kituo cha polisi uwanja wa Entebbe.
Vile vile, Jeshi la Polisi nchini humo limesambaza askari polisi kwenye barabara ya kutoka Kampala kuelekea Entebbe, ambayo inasadikika wafuasi wa Bobi Wine watakusanyika kumpokea mbunge huyo.
Bobi Wine anakabiliwa na mashtaka ya uhaini kufuatia tuhuma za kuhusika katika tukio la kupigwa mawe msafara wa Rais Yoweri Meseveni wakati wa kampeni ya uchaguzi mdogo.
Leave a comment